2013-03-15 08:25:59

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya tano ya Kipindi cha Kwaresima


Tunaendelea na tafakari Neno la Mungu Dominika ya V ya Kipindi cha kwaresima mwaka C, Mama Kanisa ametuwekea Neno ambalo linazidi kusisitiza kuhusu Huruma na Msamaha wa Mungu kwa walio wakosefu. RealAudioMP3

Dominika zilizopita tuliongozwa na Injili ya Mt. Luka na Dominika hii sehemu ya Injili yatoka katika Injili ya Mt Yohane. Katika sehemu hii ya Injili tunamwona Bwana ambaye anakwenda mlima wa mizeituni wakati wa usiku, ni katika mpango wa kuunganika na Baba yake aliye mbinguni kwa njia ya sala.

Kisha maandalizi hayo tunamwona yuko hekaluni akifundisha. Ghafla akifundisha Mafarisayo na Waandishi wanamleta mbele yake mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, wakitaka aadhibiwe vikali kadiri ya torati. Lengo lao ni kumjaribu Bwana waone anasemaje katika hili ili wapate namna ya kumshitaki. Bwana akijua hila zao anasema asiye na dhambi awe wa kwanza kumpiga mawe mama huyu. Kila mmoja aliondoka kwa upole baada ya kusutwa na hali yao ya ndani!

Mpendwa msikilizaji, Mwinjili anataka tutambue na kumfuasa Bwana ambaye anasali na kung’amua shida za watu. Bwana atatambua kwanza shida ya mama huyu aliyefumaniwa na ataona hali yake ya ndani na kisha atakuza moyo wa toba wa mama huyu na kisha atamwambia umesamehewa usitende dhambi tena. Huu ni wito mkubwa kwetu ambao kila mara tunakuzwa katika moyo wa toba na tunasamehewa dhambi zetu, tukialikwa kutotenda dhambi tena, na kujikabidhi mikononi mwa Bwana.

Bwana atang’amua shida za Mafarisayo na Waandishi, yaani unafiki wao na kukosa utambuzi wa kuwa sisi sote tunaihitaji msamaha na huruma ya Mungu. Mwanamke aliyefumaniwa alibaki na Bwana baada ya wengine kutoweka, hapa Mwinjili ataka kutuambia kuwa katika shida zote, wengine watakimbia na tutabaki na Mungu anayetupenda katika hali tuliyonayo, tuwe wadhambi kama mama huyu au wema.

Mpendwa msikilizaji, katika mateso kama tulivyosema tutabaki na Bwana aliye mwenye upendo na huruma isiyopimika. Jambo hili tunalipata pia katika somo la I Nabii Isaya anapowaambia Wana wa Israeli akisema Mungu afanyaye njia katika bahari na kuzima jeshi la adui mfano wa utambi hawezi kuwaacha kamwe. Anazidi kusema atatenda neno jipya na kufanya njia jangwani na mito ya maji nyikani.

Kwa hakika Nabii Isaya yuko katika maono anaona jinsi Mungu anavyowatoa katika utumwa wao huko Babeli. Anawafundisha Waisraeli wasiyakumbuke mambo ya zamani bali fadhila na zawadi anazowapa kwa sasa yaani uhuru kamili. Anawakumbusha jinsi Mungu alivyowatoa katika utumwa huko Misri ndivyo ambavyo upendo wake bado ulivyo na hautakuwa na mwisho.

Mtume Paulo anapowaandikia Wafilipi anawafundisha kumtazama Kristu aliye chanzo na mwisho wa maisha yao. Mtume Paulo akitaka kukazia ukuu wa Bwana, anasema kwake yeye mambo yote ya kidunia ni hasara isipokuwa kumjua Kristu. Anakuja na lugha kali kidogo akisema mambo yote ni kama kinyesi isipokuwa kumjua Kristu.

Hata hivyo anaacha nafasi ya unyenyekevu akisema si kwamba nimekwishakuwa mkamilifu bali bado nakaza mwendo ili nilipate lile ambalo kwalo nimeshikwa na Kristu. Huu ni ushuhuda wa hali ya juu wa kukiri Neno la Mungu kwa umahiri na umakini wa hali ya juu. Mkristo wewe, unapaswa kuwa ushuhuda mbele ya mataifa kama Mtume Paulo. Hata hivyo ni ngumu kumbe unahitaji kuwa na moyo mchanga ambao haujaharibiwa na chafuzi za dunia, ili uweze kupokea mambo mapya ya Kikristo.

Mpendwa mwana wa Mungu, Yesu Kristo ndiye mfano wetu hai na ndiye taa ya kutuongoza. Mtume Paulo anatoka katika hali ya ufarisayo anauchuchumalia ukristu kwa neema ya Mungu kwa ushujaa. Kuwa mkristu kunadai kujinasua kwa namna ya pekee tena ya juu, kuacha tamaduni fulanifulani ambazo zaweza kuzuia mapenzi ya Mungu.

Tunaalikwa katika Dominika hii kuwa makini kuepuka kushabikia makosa ya wengine, kuacha kutazama wengine katika mlengo wa fitina bali mlengo wa upendo ambao husamehe daima hata kama dhambi yatisha kama nini! Basi mpendwa nikutakie Kwaresima njema iliyojaa toba na msamaha daima. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.