Changamkieni masomo, dunia leo hii ni tambara bovu!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amewataka
wanafunzi wa vyuo vikuu nchini kuachana na siasa na uhanarakati na kuelekeza nguvu
yao kwenye masomo kwa sababu hayo ni mambo yanayowapoteza muda wa masomo na kuwa suala
la kufaulu ama kufeli ni suala binafsi na wala halina ubia na mtu mwingine. “Nawasihi
mjiepushe na mambo yanayowapungumzia muda ama kuwaondoa katika shughuli ya msingi
iliyowaleta hapa ya kujifunza, ili mpate digrii katika fani mliyochagua wenyewe kuisomea.
Vishawishi ni vingi na watu wanaopanga kuwashawishi ni wengi lakini lazima mkumbuke
lililowaleta chuoni,” Rais Kikwete amesema hayo, Alhamisi, Machi 14, 2013, mjini Morogoro.
Rais Kikwete alikuwa anazungumza na wana Jumuiya ya Chuo Kikuu na wananchi walioko
jirani na chuo hicho baada ya kuweka jiwe la msingi katika Jengo la Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano (ICT) na kufungua rasmi Jengo la Kitivo cha Sayansi kwenye Chuo
Kikuu cha Waislamu cha Mororgoro (MUM) kwenye eneo la Msamvu mjini Morogoro. Rais
amewaambia wanajumuiya hiyo: “Mwanafunzi wa Chuo Kikuu ni mtu mzima. Si mtoto. Lazima
mjue kuwa mnawajibika kwa kila unaloliamua na kulitenda. Amua kuwajibika vizuri. Fikiri
kabla ya kutenda. Changanua lipi la kufanya. Wakati wote uongozwe na busara na hekima
na siyo na jazba au ushabiki na matakwa ya kundi.” Ameongeza Rais Kikwete: “Kama
ni jema fanya na kama siyo jema usifanye. Lazima ujue kuwa hatma ya yote uko peke
yako. Katika masomo unanufaika wewe. Utafaulu ama kufeli wewe. Utapata shahada wewe
na siyo mtu mwingine. Hakuna ubia wa kufaulu ama kufeli ama kiwango cha kufaulu.”
Amesisitiza Rais Kikwete: “Shirikiana na wengi lakini usisahau kujali maslahi
yako. Mengi ya wengi yasiyojumuisha yako yahoji vizuri kabla ya kuamua kushiriki au
kufanya. Vinginevyo labda kama umeamua kujitoa muhanga, uwe shujaa. Hata kwa hilo,sijui
utakuwa shujaa na nani? Kama unaamua kuwa shujaa kwa kushiriki siasa na uhanarakati,
shauri yako.” Mapema, Rais Kikwete aliweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa awamu
ya kwanza ya Jengo la ICT na pia kuzindua rasmi Jengo la Kitivo cha Sayansi kwenye
Chuo Kikuu hicho ambacho ni moja ya vyuo vya juu 68 nchini. Makamu wa Mkuu wa
Chuo hicho, Profesa Hamza Mustafa Njozi amemwambia Rais Kikwete kuwa awamu ya kwanza
ya ujenzi wa Jengo la ICT mpaka sasa imegharimi kiasi cha dola za Marekani 350,000,
sawa na asilimia 16 ya gharama zote za ujenzi, ambazo zimetolewa kama msaada na Benki
ya Maendeleo ya Kiislam ya Islamic Development Bank (IDB) yenye makao yake Saudi Arabia.
Profesa Njozi amesema kuwa jengo la Kitivo cha Sayansi limegharimu sh milioni
450 na wanafunzi wapatao 500 wananufaika na kujengwa kwa jengo hilo jipya. Kundi la
kwanza la wananchi hao lilimaliza masomo yao Novemba, mwaka jana, 2012. MUM ambacho
kinaendeshwa na taasisi ya mfuko wa Kiislamu iitwayo Muslim Development Fund (MDF)
kilianzishwa kutoa masomo mwaka 2005 baada ya Rais Benjamin Mkapa kutoa majengo yaliyokuwa
ya Chuo cha Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa MDF kwa madhumuni ya kuanzisha
chuo hicho kikuu cha kwanza kuendeshwa na Waislam nchini. Idadi ya wanafunzi wa
chuo hicho imeongezeka kutoka 167 miaka saba iliyopita katika mwaka wa kwanza wa 2005
hadi kufikia 2,678 wa sasa ambao kati yao 1,571 ni wanaume. Kwa sasa chuo hicho kina
wahadhiri wa kudumu 45 na wahadhiri wa muda 50. JK: Tulipanua elimu kwa sababu
tulikuwa nyuma Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya
Mrisho Kikwete amesema kuwa Serikali yake iliamua kupanua kwa kiwango kikubwa elimu
nchini kwa ngazi zote kwa sababu Tanzania ilikuwa nyuma sana ya nchi nyingine jirani
katika sekta ya elimu miaka saba iliyopita. Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali
yake ilichukua uamuzi huo wa busara kwa sababu vijana wengi wa Tanzania waliostahili
kupata elimu ya awali, msingi, sekondari, ufundi na elimu ya juu walikuwa hawaipati
elimu hiyo. Rais Kikwete ameyasema hayo, Alhamisi, Machi 14, 2013, wakati alipohutubia
wanajumuiya ya Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro (MUM) na wananchi wanaoishi jirani
na chuo hicho baada ya kuweka jiwe la msingi kwenye Ujenzi wa Jengo la Teknolojia
ya Habari na Mawasiliano (ICT) na kufungua Jengo la Kitivo cha Sayansi kwenye chuo
hicho kwenye eneo la Msamvu, mjini Morogoro. Rais Kikwete amewaambia wananchi
hao: “Katika Kipindi cha miaka saba, Serikali yetu imeongeza sana uwekezaji katika
upanuzi wa elimu tangu ya awali hadi elimu ya juu. Tuliamua kufanya hivyo kwa sababu
vijana wengi waliokuwa wanastahili kupata elimu ya awali, msingi, sekondari, ufundi
na elimu ya juu walikuwa hawaipati.” Ameongeza: “Tanzania ni kubwa mara mbili
kuliko Kenya na mara tatu kuliko Uganda kwa eneo na idadi ya watu lakini sisi ndiyo
tulikuwa na idadi ndogo zaidi ya wanafunzi katika ngazi hizo zote. Kwa mfano, mwaka
2005, idadi ya wanafunzi waliokuwa Chuo Kikuu nchini Kenya ilikuwa 108, 407, Uganda
88,360, na baadhi ya nchi za SADC kama vile Afrika Kusini idadi hiyo ilikuwa 717,
973. Wakati wenzetu walikuwa na idadi hiyo, sisi tulikuwa na wanafunzi 40, 719 tu
katika vyuo vikuu nchini.” Amesisitiza Rais Kikwete: “ Hali hiyo ilikuwa pia kwa
elimu ya sekondari. Kenya ilikuwa na wanafunzi 925,341, Uganda 619,519 na Afrika Kusini
4,186,882 wakati Tanzania ilikuwa na wanafunzi 524,325 tu waliokuwa katika shule za
sekondari. Hali hii haikukubalika na tukaamua hatuwezi kuiachia iendelee. Tukachukua
hatua tulizozichukua.” Rais Kikwete amesema kuwa matokeo ya uamuzi ni kwamba vijana
wengi wa Tanzania leo wanapata fursa kubwa zaidi za elimu kuliko wakati wowote katika
“historia ya nchi yetu.” Amesema kuwa sasa kazi inayoendelea ni kuimarisha ubora wa
elimu wapatayo vijana wa Tanzania kwa kuongeza idadi ya walimu, vifaa vya kufundishia
na vitabu. Ameongeza Rais Kikwete: “Kufuatia juhudi hizo, idadi ya wanafunzi waliopo
kwenye vyuo vikuu nchini imeongezeka sana, kutoka wanafunzi 40,719 mwaka 2005 hadi
kufikia 166,484 mwaka 2012. Kwa upande wa sekondari mwaka 2011 tulikuwa na wanafunzi
milioni 1.79 na wenzetu wa Kenya walikuwa na wanafunzi 1.77. Haya ni mafanikio makubwa
na Serikali itaendelea kuwekeza katika upanuzi wa fursa za elimu na ubora wake.” Rais
Kikwete pia amesifu, kupongeza na kuwashukuru wadau wengine wa elimu ambao wametoa
mchango mkubwa katika kupanua fursa ya elimu kwa vijana wa Tanzania. “Kwa mfano, katika
vyuo vikuu 49 vilivyopo nchini kwa sasa, vinavyomilikiwa na umma ni 14 tu. Vyuo vikuu
24 vinamilikiwa na mashirika ya dini na 11 ni vya sekta binafsi.”