Baba Mtakatifu Francis ni Myesuiti wa kwanza kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni Papa
wa kwanza katika historia ya Kanisa kutoka nje ya Bara la Ulaya na Papa wa kwanza
katika historia ya Kanisa kutoka katika nchi za Amerika ya Kusini, nchi ambazo kwa
sasa zina idadi kubwa ya waamini wa Kanisa Katoliki. Kwa mara ya kwanza Jina la Mtakatifu
Francis linatumiwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Lakini ikumbukwe kwamba,
kuna watakatifu wanne wenye majina ya Francis. Hawa ni akina Mtakatifu Francis wa
Assisi, Msimamizi wa Italia; Mtakatifu Francis wa Sale, Mwalimu wa Kanisa na Msimamizi
wa Waandishi wa Habari; Mtakatifu Francis Xsaveri, Myesuit na Msimamizi wa Wamissionari
pamoja na Mtakatifu Francis wa Paulo, Mkaa pweke na mwanzilishi wa Shirika la Ndugu
wadogo wa Calabria.
Kardinali Jorge Mario Bergoglio, SJ, Askofu mkuu wa Jimbo
kuu la Buenos Aires, Argentina, alizaliwa tarehe 17 Desemba 1936 mjini Buenos Aires.
Yeye ni mtoto wa Mzee Mario na Mama Regina Sivori, waliobahatika kupata watoto watano.
Katika ujana wake, alisoma na kufuzu kama mtaalam wa kemia, baadaye akaacha kazi hii
na kujiunga Seminarini huko Villa Devoto.
Tarehe 11 Machi 1958 alijiunga na
malezi ya Kinovisi katika Shirika la Wayesuit akaendelea pia na masomo dunia nchini
Cile na kunako mwaka 1963 alirejea tena Buenos Aires na kujipatia shahada ya uzamili
kutoka katika Kitivo cha Falsafa, Chuo Kikuu cha San Josè huko San Miguel.
Kati
ya mwaka 1964 na mwaka 1965 alikuwa ni Jaalim wa Fasihi Andishi na Saikolojia katika
Chuo cha Bikira Maria wa Santa Fe. Kunako mwaka 1966 akafundisha masomo haya kwenye
Chuo Kikuu cha Salvatore cha Buenos Aires. Kuanzia mwaka 1967 hadi mwaka 1970, alijiendeleza
kwa masomo ya Taalimungu katika Chuo Kikuu cha San Josè kilichoko San Miguel na kujipatia
shahada ya uzamili.
Tarehe 13 Desemba 1969 akapewa daraja takatifu la Upadre.
Kati ya mwaka 1970 hadi mwaka 1971 alikamilisha hatua ya tatu ya majiundo yake kama
Myesuit huko Hispania na tarehe 22 Aprili 1973 akaweka nadhiri za daima. Kati ya mwaka
1972 hadi mwaka 1973 alikuwa ni mlezi wa Wanovisi, Jaalim, Mshauri na Gombera wa Chuo
cha Massimo. Tarehe 31 Julai 1973 akateuliwa kuwa Mkuu wa Jimbo la Argentina kwa upande
wa Shirika, utume ambao aliutekeleza kwa muda wa miaka 6. Kati ya Mwaka 1980 hadi
mwaka 1986, alikuwa ni Gombera wa Chuo cha Massimo na Paroko wa Parokia ya Patriaki
San Josè, Jimboni San Miguel.
Kunako mwaka 1986 alikwenda nchini Ujerumani
kumalizia masomo yake katika Shahada ya Uzamivu na wakuu wake wa Shirika wakampatia
jukumu la kuwa mkuu wa malezi ya kiroho na muungamishi katika Chuo cha Salvatore.
Tarehe
20 Mei 1992 Papa Yohane Paulo II akamteuwa kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Buenos
Aires, akawekwa wakfu kama Askofu tarehe 27 Juni 1992. Tarehe 3 Juni 1997 akateuliwa
kuwa Askofu mwandamizi wa Jimbo kuu la Buenos Aires na tarehe 28 Februari 1998 akasimikwa
kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires baada ya kifo cha Kardinali Antonio
Quarracino na hivyo kuwa pia ni Mkuu wa Kanisa Katoliki Argentina.
Mwenyeheri
Yohane Paulo II akamteuwa na kumsimika kuwa Kardinali kunako tarehe 21 februari 2001.
Ameshiriki katika Sinodi ya Maaskofu iliyofanyika kunako mwaka 2001. Akashiriki pia
kwenye mkutano wa Makardinali wakati wa uchaguzi wa Papa kati ya tarehe 18 na 19 Aprili
2005. Alikuwa ni mjumbe wa Halmashauri ya Sinodi ya kumi na moja ya Maaskofu kuanzia
tarehe 2 hadi 23 Oktoba 2005.
Mjini Vatican alikuwa ni mjumbe wa Baraza la
Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa, Baraza la Kipapa kwa ajili ya
Makleri, Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Tume ya Kipapa
ya Amerika ya Kusini, Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri na Mjumbe wa Sekretarieti
ya Sinodi.
Nchini Argentina alikuwa ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Argentina. Rais
wa Tume ya Baraza la Maaskofu kwa ajili ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Argentina. Alikuwa
ni mratibu mkuu wa Mahakama ya Kanisa; Mratibu wa Mahakama ya Jimbo kuu la Buonos
Aires. Tangu mwaka 2005 hadi 2011 alikuwa ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina. Ni
mwandishi wa Vitabu vifuatavyo:
1982: Meditaciones para
religiosos 1986: Reflexiones sobre la vida apostólica 1992: Reflexiones
de esperanza 1998: Diálogos entre Juan Pablo II y Fidel Castro 2003:
Educar: exigencia y pasión 2004: Ponerse la patria al hombro 2005:
La nación por construir 2006: Corrupción y pecado 2006: Sobre
la acusación de sí mismo 2007: El verdadero poder es el servicio