2013-03-14 07:42:08

Ratiba elekezi ya Baba Mtakatifu Francis!


Ifuatayo ni ratiba elekezi ya Baba Mtakatifu Francis anapoanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Tarehe 14 Machi 2013, Baba Mtakatifu asubuhi anatembelea kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu. Hii ni hija binafsi ya kiroho kwa heshima ya Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa.Alipofika kanisani hapo, alisali kwa kitambo kidogo na baadaye akaondoka, akiwa ameandamana na baadhi ya viongozi waandamizi wa nyumba ya kipapa.

Alhamisi, tarehe 14 Machi 2013, Majira ya jioni saa 11:00 Jioni kwa saa za Ulaya, Baba Mtakatifu Francis ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na Makardinali walioshiriki kwenye uchaguzi wa Papa Mpya. Ibada hii inaadhimishwa kwenye Kikanisa cha Sistina, mahali ambapo Makardinali walikuwa wanafanyia uchaguzi.

Ijumaa, tarehe 15 Machi 2013, Majira ya saa 5:00 asubuhi, Baba Mtakatifu Francis atakutana na kuzungumza na Makardinali wote.

Jumamosi tarehe 16 Machi 2013 Baba Mtakatifu atakutana na kuzungumza na Waandishi wa Habari kutoka sehemu mbali mbali za dunia ambao wako hapa mjini Vatican kuhabarisha ulimwengu yale yanayojiri wakati huu pamoja na kuwashukuru kwa kazi kubwa waliyoifanya. Mkutano huu na wanahabari utafanyika kwenye ukumbi wa Paulo wa sita, hapa mjini Vatican.

Jumapili, tarehe 17 Machi 2013, Baba Mtakatifu Francis, kwa mara ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, atasali na waamini, mahujaji na wageni watakaofika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican Sala ya Malaika wa Bwana.

Jumanne, tarehe 19 Machi 2013, Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu, Baba Mlishi wa Yesu, Papa Francis ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Hapa utakuwa ni mwanzo rasmi wa utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Katika Ibada hii ya Misa Takatifu Makardinali watarudia kula kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ibada hii inatarajiwa kuanza saa 3:30 kwa saa za Ulaya.

Jumatano tarehe 20 Machi 2013, Baba Mtakatifu Francis, atakutana na kuzungumza na wawakilishi kutoka sehemu mbali mbali za dunia watakaokuwa wamefika hapa mjini Vatican kwa ajili ya tukio hili. Ratiba elekezi inaonesha kwamba, Jumatano ijayo, hakutakuwa na Katekesi ambayo kwa kawaida inatolewa na Baba Mtakatifu kila siku ya Jumatano.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itaendelea kuwa nawe bega kwa bega katika matukio yote haya!







All the contents on this site are copyrighted ©.