2013-03-14 08:12:49

Papa Francis anawashukuru na kuwaomba waamini kusali kwa ajili yake na Kanisa!


Bahari ya waamini, mahujaji na watalii ilifurika Jumatano Usiku, wakati waliposikia kengele za Kanisa kuu la Mtakatifu Petro zikipigwa na moshi mweupe ukiendelea kutoka kwenye paa la Kikanisa cha Sistina, ishara kwamba, Kanisa limempata Khalifa wa Mtakatifu Petro, ambaye tangu sasa anajulikana kama Francis RealAudioMP3

Wakati akitoa baraka zake za kichungaji kwa mji wa Roma na Dunia kwa ujumla, "Urbi et Orbi" alisema kwamba, Makardinali katika mkutano wao wa uchaguzi wamefunga safari ndefu hadi miisho ya dunia ili kuwapatia Askofu wa Roma. Kwanza kabla ya yote, aliomba sala kutoka kwa waamini na kila mtu mahali alipokuwa alisimama kwa kitambo kidogo ili kusali na kumwombea Baba Mtakatifu Francis.

Amewashukuru kwa makaribisho ya nguvu na kwa namna ya pekee, aliwaomba waamini na mahujaji waliokuwa wamemiminika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro pamoja na viunga vyake, kusali kwa ajili ya kumwombea Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita.

Baada ya sala hii, Baba Mtakatifu Francis, aliwaambia waamini kwamba, kwa sasa wakiwa wanaandamana na Askofu wao, wanaanza hija ya Kanisa la Roma ambalo ni kielelezo cha upendo kwa Makanisa yote. Hii ni hija ya mshikamano wa kidugu na imani miongoni mwa watu wa Familia ya Mungu. Amewashukuru viongozi mbali mbali wa Kanisa watakoshirikiana naye katika mwendelezo wa mchakato wa Uinjilishaji mpya, kwa Mji wa Roma.

Kwa mara nyingine Baba Mtakatifu Francis aliomba sala kwa waamini waliokuwa wamekusanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro na baadaye akatoa baraka ya kitume "Urbi et Orbi".







All the contents on this site are copyrighted ©.