2013-03-13 11:02:58

Moshi mweupe tayari! PAPA MPYA! SUBIRI KIDOGO


Makardinali 115 wenye dhamana ya kupiga na kupigiwa kura, Jumatano, tarehe 13 Machi 2013, baada ya maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, waliingia kwenye Kikanisa cha Sistina kwa ajili ya kusali masifu ya asubuhi na baadaye wakaendelea na mchakato wa kupiga kura.

Leo Makardinali wanatarajia kupiga kura mbili asubuhi na mbili jioni. Wakati wote huu, macho na masikio ya waamini na watu wenye mapenzi mema yanaendelea kuelekezwa kwenye Paa la Kikanisa cha Sistina, kitakachotoa alama ya moshi mweupe alama ya kwamba Kanisa limempata Papa Mpya; moshi mweusi, alama kwamba, mchakato bado unaendelea!

Waamini wanakumbushwa kwamba, uchaguzi wa Papa ni tofauti kabisa na uchaguzi unaofanywa katika medani za kisiasa au katika uchaguzi wa mkurugenzi mkuu wa Shirika la Kimataifa. Hapa Makardinali wamekusanyika kwa ajili ya kumchagua Kiongozi wa Kanisa, atakayepewa dhamana ya kuongoza Jumuiya ya Waamini. Kumbe, yule atakeyechaguliwa kwanza kabisa hana budi kuwa na sifa njema za maisha ya kiroho: mchamungu, anayejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili kutangaza kweli za Kiinjili, mtu anayeaminika na kukubalika na Kanisa na Jamii ya watu wanaomzunguka.

Conclave ni kipindi maalum cha imani, matumaini, mapendo na mshikamano miongoni mwa Makardinali na Kanisa kwa ujumla, ndiyo maana Waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kuwasindikiza Makardinali katika sala. Conclave ni tukio la Liturujia ya Kanisa inayoadhimishwa kwenye Kikanisa cha Sistina, chenye utajiri mkubwa wa sanaa, kinachotoa fursa kwa Makardinali: kusali na kutafakari maajabu na ukuu wa Mungu, wakitambua dhamana waliyokabidhiwa na Kanisa ya kuchagua Kiongozi mkuu.

Hapa hakuna mgawanyiko kama baadhi ya wanahabari wanavyotaka kuwaaminisha wasomaji, watazamaji na wasikilizaji wao! Katika mikutano elekezi, Makardinali wamezungumza katika ukweli na uwazi; mwanga wa Kanisa na Vivuli vinavyoliandama Kanisa; yote haya yamefanyika katika matumaini, utulivu wa ndani na uhuru kamili. Makardinali wakikamilisha mchakato wa uchaguzi, ulimwengu utafahaamishwa mara moja!

Itakumbukwa kwamba, kila siku, Makardinali kadiri ya Misale ya Conclave, wanaweza kuchagua nia ya misa moja kwa ajili ya mahitaji ya Kanisa: kwanza kabisa kwa kufuata liturujia ya siku; kumwomba Roho Mtakatifu; kusali kwa ajili ya Kanisa zima; kumwomba Bikira Maria au kusali kwa ajili ya maombezi ya Watakatifu Petro na Paulo.







All the contents on this site are copyrighted ©.