Kuanzia Mtaguso wa Kwanza wa Yerusalemu kama inavyobainishwa kwenye Kitabu cha Matendo
ya Mitume: 15: 14- 17: Yakobo akajibu akisema, “Ndugu zangu, nisikilizeni. Simeoni
ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika
hao kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya Manabii yanapata na hayo, kama ilivyoandikwa:
Baada ya mambo haya nitarejea, nami nitaijenga tena nyumba ya Daudi iliyoanguka. Nitajenga
tena maanguko yake, nami nitaisimamisha, ili wanadamu waliosalia wamtafute Bwana,
na mataifa yote ambayo jina langu limetajwa kwao, asema Bwana, ajulishaye hayo tangu
milele.” Injili ya Luka inasimulia “Tazama mimi niko kati yenu kama yule anayehudumia”
Lk. 22:24-27. Maandiko Matakatifu yanaonesha maana halisi ya Kibiblia mintarafu uchaguzi
wa Papa unaofanywa na Dekania ya Makardinali. Kanisa haliwezi kuwa ndani ya Kristo
bila ya uwepo wa Mtakatifu Petro, mwamba na kiongozi wa Kanisa; Mtume Petro si kiongozi
anayehudumia katika upweke, bali kwa njia ya mshikamano: ”Yeye ni wa kwanza na Kiongozi
wa Mitume na wengine wote ambao wako pamoja naye” Lk 24:33; Yeye ni kiini cha umoja
wa wale wote wanaomfuasa Kiongozi mkuu 1Pt. 5:4, Ni Kiongozi mkuu wa viongozi wote
wa Watu wa Mungu. Kiongozi huyu mkuu ni ”Sakramenti wazi” katika kipindi chochote
kile cha historia na hata kwa wakati huu, Mtakatifu Petro daima anajipambanua kwa
kuwa na mshikamano na wengine na wote wanaomzunguka Mtakatifu Petro.