2013-03-12 13:18:23

Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kielelezo cha Upendo, Umoja na Mshikamano wa Kanisa


Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali, Jumanne tarehe 12 Machi 2013 ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kwa ajili ya kuombea uchaguzi wa Papa Mpya, kielelezo makini cha upendo, umoja na utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Waamini wamekusanyika kwa ajili kumwabudu, kumshukuru na kumwomba Mwenyezi Mungu, ambaye kwa njia ya upendo wake ameendelea kulisimamia, kuliongoza na kuliimarisha Kanisa kwa njia ya Roho Mtakatifu.

Kardinali Sodano amemshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa uongozi wake makini kwa Kanisa na kwamba, sasa Makardinali wanaanza uchaguzi wa Papa wa 265. Kanisa linamwomba Mwenyezi Mungu aweze kulikirimia Kiongozi mwema kwa ajili ya Kanisa lake. Huyu ndiye anayetumwa kuwahubiria wanyenyekevu Habari Njema ya Wokovu; kuwaganga wale waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari ya kufunguliwa kwao, kutangaza Mwaka wa Bwana uliokubalika.

Kardinali Sodano anasema kwamba, utabiri huu umepata utimilifu wake kwa njia ya Yesu Kristo, aliyekuja kuwaonjesha watu upendo wa Mungu, kwa wote wanaoteseka, wanaokabiliana na ukosefu wa haki msingi za binadamu, umaskini pamoja na kumong'onyoka kwa maadili na utu wema. Wote hawa wanahitaji kuona huruma ya Mungu, utume ambao unatekelezwa na viongozi wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee na Khalifa wa Mtakatifu Petro, ambaye baada ya kuonesha upendo mkuu kwa Kristo, alikabidhiwa dhamana ya kuwachunga Kondoo wake. Hii ni huduma ya upendo inayotekelezwa mintarafu mwanga wa Injili na nguvu ya neema.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Ujumbe wake wa Kwaresima kwa Mwaka 2013 alibainisha kwamba, kilele cha matendo ya huruma kinajionesha kwa njia ya Uinjilishaji; yaani huduma ya Neno la Mungu pamoja na adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu, linalowahusisha na kuwachangamotisha Watu wa Mungu kujenga na kuimarisha uhusiano na Muumba wao.

Uinjilishaji ni kielelezo cha hali ya juu kabisa cha huduma kwa binadamu na kwamba, Yesu Kristo ni nguzo msingi katika mchakato wa maendeleo endelevu, kama alivyobainisha Papa Paulo wa sita, katika Waraka wake juu ya Maendeleo ya Watu.

Kardinali Angelo Sodano anasema kwamba, Neno la Mungu limefafanua kwa dhati kabisa juu ya Fumbo Kristo na Kanisa lake; umuhimu wa kujenga na kuimarisha umoja wa Kanisa, kila mtu kadiri ya karama aliyopokea, akitekeleza wajibu wake katika fadhila ya upendo na amani. Umoja huu unasimikwa katika utofauti wa karama na majukumu, lakini kwa pamoja unapania kujenga na kuimarisha Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.

Huu ndio umoja unaojengwa na kuimarishwa na Roho Mtakatifu na kwamba, Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kielelezo wazi cha umoja wa Kanisa, changamoto kwa kila mwamini kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa umoja wa Kanisa.

Kardinali Sodano anasema amri kuu ambayo Kristo aliwaachia mitume wake, ile siku iliyotangulia kuteswa kwake ni upendo. Huu ndio mhimiri mkuu wa Viongozi wa Kanisa, wanaosukumwa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ndugu zao katika Kristo. Huu ni wajibu mkubwa kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro anayepaswa kuonesha upendo huu kwa Kanisa zima anapotekeleza wajibu wake wa kuwaongoza Watu wa Mungu na Ulimwengu katika ujumla wake, daima akitafuta kudumisha na kuimarisha misingi ya haki na amani.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema, huduma ya upendo ni asili, utume na utambulisho wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee, Kanisa la Roma, ambalo kimsingi ni kielelezo cha upendo. Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali anahitimisha mahubiri yake kwa kuwaalika waamini kusali kwa ajili ya kuombea mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya, atakayetekeleza utume huu nyeti katika Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.