2013-03-09 11:05:42

Kanisa Katoliki Tanzania linaendelea kutimua vumbi katika sekta ya elimu ya juu!


Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican wakati huu Kanisa Katoliki nchini Tanzania linapoadhimisha Miaka 150 tangu Wamissionari wa kwanza walipotua Visiwani Zanzibar, huo ukawa ni mlango wa Imani kwa Kanisa Katoliki, linajivunia mchango wake katika sekta ya elimu nchini Tanzania. RealAudioMP3

Anasema, kwa hakika Kanisa limekuwa ni mdau mkuu wa maendeleo ya elimu nchini Tanzania kuanzia katika shule za awali, msingi, sekondari, vyuo na sasa linaendelea kucharuka katika mchakato wa maboresho ya elimu ya juu. Hii ni changamoto iliyotolewa na Mapadre, Watawa na Waamini waliokerwa na uduni wa elimu ya Tanzania kwa wakati huo, wakaamua kulivalia njuga tatizo hili kwa kuwekeza katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augostino cha Tanzania, SAUT, leo hii, anasema Askofu mkuu Lebulu, kinatimua vumbi nchini Tanzania! Wengi walidhani kwamba, hii ilikuwa ni nguvu ya soda, lakini matunda yake yanaendelea kujionesha sehemu mbali mbali za Tanzania.

Alipohojiwa kuhusu "siri ya mafanikio haya" Askofu Mkuu Lebulu hakusita kusema kwamba, ni jeuri, ari na hamasa iliyotolewa na Mapadre pamoja na Watawa walioamua kwa dhati kabisa kuwekeza katika uongozi bora, wakitafuta mafao ya watanzania wengi; wakaonesha mipango na mikakati endelevu kwa ajili ya maboresho ya sekta ya elimu ya juu nchini Tanzania. Wakatafuta, wakakusanya na kuzalisha fedha kwa ajili ya ustawi wa elimu Tanzania. Fedha hii imetumika barabara na matokeo yake ni kuendelea kupanuka kwa SAUT sehemu mbali mbali za Tanzania!

Hawa ni Mapadre waliotambua na kudhamiria kuendesha sekta ya elimu chini ya uongozi na usimamizi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kwa kuongoza kisayansi na hivyo kuingia katika ushindani wa soko la elimu ya juu kisayansi, wakiwa na lengo la kuwapatia watanzania wenzao elimu iliyo bora zaidi, itakayowasaidia kupambana na mazingira yao, ili Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla, iwe ni mahali pazuri zaidi pa kuishi!

Askofu mkuu Josephat Lebulu anakiri kwamba, Kanisa Katoliki nchini Tanzania lilisinzia kidogo katika kuwekeza kwenye mfumo wa elimu ya juu, lakini baada ya kutambua umuhimu wake, leo hii linaendelea kutimua vumbi! SAUT, haishikiki!







All the contents on this site are copyrighted ©.