2013-03-09 08:27:54

Camerlengo na kazi zake


Kuanzia karne ya kumi na moja, historia ya Kanisa Katoliki inaonesha kwamba, kulikuwepo na kiongozi aliyejulikana kama “Camera thesauraria” “Mhazini wa Kanisa” aliyepewa dhamana ya kuratibu masuala ya fedha na mali ya Kanisa.

Dhamana hii kwa sasa inatekelezwa wakati ambapo kiti cha ukulu wa Mtakatifu Petro kiko wazi, kama ilivyo kwa wakati huu, baada ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kung’atuka kutoka madarakani hapo tarehe 28 Februari 2013.

Kunako Karne ya 12 mkuu wa Ofisi hii alijukana kama “Camerarius” au Camerlengo. Kadiri ya miaka ilivyozidi kuyoyoma, Camerlengo ambaye kwa Kiswahili chepesi tungeweza kusema, “Mlinzi” au “Mratibu” akapewa dhamana kuwa Katibu mkuu wa shughuli za Kanisa pamoja na kushughulikia masuala ya sheria na kesi mbali mbali. Ni kiongozi aliyekuwa juu ya Mahakama zote zilizokuwa chini ya Vatican.

Tarehe 29 Juni 1908 Papa Pio wa tisa, katika Waraka wake wa kichungaji “Sapienti Consiglio” akamrudishia Caerlengo madaraka aliyokuwa nayo kwa miaka iliyopita, yaani kusimamia fedha na mali ya Kanisa wakati ambapo kiti cha ukulu wa Mtakatifu Petro kiko wazi.

Kunako mwaka 1967 Papa Paulo wa sita, katika Waraka wake wa kichungaji “Regimi Ecclsiae Universe, alibainisha kwamba, ikiwa kama Camerlengo anazuiliwa kutekeleza wajibu wake kisheria, basi msaidizi wake afanye kazi kuanzia pale ambapo kiti cha ukulu wa Mtakatifu Petro kiko wazi hadi uchaguzi wa Papa Mpya. Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili katika Waraka wake wa kichungaji “Pastor Bonus wa mwaka 1988 akathibitisha tena dhamana hii.

Kunako mwaka 1996, Papa Yohane Paulo wa Pili akatamka wazi katika Waraka wake wa kichungaji “Universi Dominici Gregis” kwamba, ni viongozi wakuu wawili tu ambao nyadhifa zao haziwezi kukoma wakati ambapo kiti cha ukulu wa Mtakatifu Petro kiko wazi. Hawa ni Camerlengo na Mhudumu mkuu wa Toba.

Itakumbukwa kwamba, kwa sasa Camerlengo ni Kardinali Tarcisio Bertone aliyeteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, tarehe 22 Juni 2006 kuwa Katibu mkuu wa Vatican. Tarehe 4 Aprili 2007 akamteuwa pia kuwa ni Camerlengo. Kwa mara ya kwanza, alianza kutekeleza wajibu wake huu nyeti, tarehe Mosi, Machi 2013 baada ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kung’atuka kutoka madarakani.

Mkaguzi mkuu msaidizi wa fedha na mali ya Kanisa ni Askofu Giuseppe Sciacca, ambaye naye anajulikana kama Camerlengo msaidizi. Viongozi hawa wawili wanasaidiwa na jopo la Dekania ya Mapadre wanane. Ni matumaini ya Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican kwamba, walau kwa sasa umeweza kupata fununu yak ile kinachoendelea ndani ya Kanisa wakati huu Kanisa linaposali kwa ajili ya kuwaombea Makardinali ili waweze kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro, atakayeliongoza Kanisa katika kipindi hiki cha mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Makala hii imeandaliwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.