2013-03-08 16:15:26

Habari kutoka Kikao cha Saba cha Makardinali


Waadhama Makardinali wanaendelea na Mkutano wao hapa Vatican , ambamo Ijumaa hii majira ya asubuhi walifanya kikao cha saba.
Mkurugenzi wa kitengo cha habari Vatican, Padre Federico Lombardi, kama kawaida yake, majira ya mchana alitoa muhtasari kwa wanahabari, juu ya yaliyofanyika katika kikao hiki cha saba cha Makardinali.
Katika maelezo yake, alionyesha uwezekano wa Makardinali kuchagua tarehe ya kuanza vikao vya kumchagua Papa, kinachoitwa Conclave. Na kwamba kuna mwelekeo mkubwa wa Conclave kuanza mapema wiki ijayo. Asubuhi hii, jumla ya Makardinali 153 walishiriki kikao , kati yao wapiga kura wakiwa 115.
Padre Lombardi alitaja baadhi ya hoja zilizojadiliwa , kwamba, ni pamoja na Katiba "Universi Dominici Gregis", ambamo walitaka kujua, sababu msingi zilizo zuia makardinali walioshindwa kuhudhuria mkutano huu. Aliwataja walioshindwa kufika ni Makardinali wawili, Kardinali Mstaafu Julius Riyadi Darmaatmadja wa Jarkata, na Kardinali O'Brien, ambao wameomba udhuru kwa kutaja sababu zilizowazuia ni pamoja na udhaifu wa mwili na pili ni sababu binafsi. Mkutano wa Makadinali ulipiga kura na kukubali sababu zilizotolewa.

Aidha asubuhi kulikuwa na vipengere 18 vilivyowasilishwa na kujadiliwa , kati yake ikiwemo mazungumzo kati ya dini, maadiliviumbe, haki katika dunia. Pia walijadili furaha ya kutangaza Injili na Huruma ya Mungu wakimrejea Mwenye Heri Papa Yohane Paulo II. Na pia walijadili hoja ya ushirikiano na umoja katika decania ya Makardinali.







All the contents on this site are copyrighted ©.