Ujumbe wa Kwaresima kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kwa Mwaka 2013
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linasema Kwaresima ni safari inayowajenga waamini
katika Imani. Maaskofu wanachambua kwa kina na mapana hali halisi ya imani. Katika
ujumbe wao, Maaskofu wanatoa pia fundisho la jumla: kwa kufafanua kuhusu imani, familia,
Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo. Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linayaangalia
matukio makuu na muhimu katika maisha na utume wao wa Kanisa. Imani katika maisha
ya kisiasa inapania kutafuta mafao ya wengi. Basi kwa muhtasari huu, Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican inakutakia tafakari njema, ukiweza washirikishe pia jirani zako!
UTANGULIZI
Wapendwa
Taifa la Mungu,
Neema na iwe kwenu na amani zitokazo kwa Mungu Baba yetu na
kwa Bwana Yesu Kristo… Macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake
jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo;
na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo… (Efe 1:2, 18-19).
“Simameni imara katika imani” tuliyoipokea kutoka kwa Mungu anayependa kutushirikisha
maisha yake ya upendo. Imani ni njia pekee inayotuongoza katika upendo na muungano
na Mungu. Ndiyo maana, sisi wachungaji wenu tunawaleteeni ujumbe huu wa Kwaresima
kama sehemu ya wajibu wetu wa msingi, ili “kumfundisha kila mtu katika hekima yote,
tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo” (Kol 1:28). Katika maadhimisho ya
Kwaresima ya mwaka huu, tunaungana na Mtume Paulo kuwahimizeni kwa msisitizo mkubwa
na wa upendo tukisema tena: “Simameni imara katika imani” (1Kor 16:13). Hii ndiyo
dira na mwaliko wa Kanisa kwa nyakati zote, na zaidi sana katika wakati wetu huu wa
kihistoria ambapo kumejitokeza sana kuyumba kwa imani miongoni mwa waamini na hivi
kuamsha uhitaji wa Uinjilishaji Mpya na wa kina kwa matendo. Tunapenda kuwashirikisha
tafakari hii ili ituongoze sisi sote katika kuishi kiaminifu imani ile tunayoishiriki
pamoja, imani ambayo baada ya kuipokea tunapaswa kuilinda, kuitunza na kuikuza. Tunataka
mtambue siku zote kuwa sisi, kwa wajibu tuliopewa na Kanisa, tunapaswa kufundisha,
kuilinda na kuifanya imani yenu ikue, na wala “si kwamba tunatawala imani yenu; bali
tu wasaidizi wa furaha yenu; maana kwa imani yenu mnasimama” (2Kor 1:24). Ni sala
yetu kuwa, katika Mwaka huu wa Imani, tutafanya bidii ya makusudi kuijua, kuiishi
na kuwashirikisha wengine imani yetu, ili “sote tuufikie umoja wa imani na kumjua
Mwana wa Mungu; tuwe watu waliokomaa na kuufikia utimilifu wake Kristo mwenyewe” (Efe
4:13). SURA YA KWANZA
KWARESIMA: SAFARI INAYOTUJENGA KATIKA IMANI “Wakati
umetimia, na Ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Habari Njema” (Mk 1:15).
Haya ndiyo maneno ya kwanza ya Yesu, ambayo kadiri ya Mwinjili Marko, yanafungua utume
wake Yesu. Hii ndiyo habari njema ya Kristo. Huo ndio msingi wa utume na muhtasari
wa utume wa Mkombozi: kuujenga Ufalme wa Mungu ndani ya mioyo ya watu na miongoni
mwa watu kupitia tendo la toba na imani.
Kipindi
cha Kwaresima ni mwaliko wa kusafiri kiroho na Kristo Mwokozi wetu, kupitia njia ya
toba na imani, ambayo kwayo mwanadamu anashiriki kuujenga Ufalme wa Mungu; ufalme
wa upendo, wa haki na wa amani. Huu ni ufalme ambao “hata hivyo lengo lake la moja
kwa moja ni usafi wa moyo, ambao bila huo hatuwezi kulifikia. Kwa hiyo tunapaswa kuwa
na lengo hili akilini, na ikitokea kwamba kwa kipindi kifupi moyo wetu unaiacha njia
hii ya moja kwa moja, tunapaswa kuirudia mara moja, tukiyaongoza maisha yetu kwa kulirejea
lengo letu.”
Kila Mwaka, Kanisa linaadhimisha fumbo la ukombozi
wetu si kama kumbukumbu tu ya yaliyopita, bali uhalisia tunaopaswa kuuishi kila siku
katika maisha yetu, na hivi kuendeleza tendo la ukombozi katika wakati wa sasa wa
historia. Katika safari ya Kwaresima, Kanisa linatuongoza kwa tafakari na mazoezi
yatakayotusaidia kukutana na Bwana Mfufuka aliye jiwe kuu la msingi la Ufalme wa Mungu.
Kristo ndiye msingi wa imani yetu, imani ambayo “ni mwaliko wa uongofu wa dhati na
ulio mpya kwa Bwana, na mwokozi pekee wa ulimwengu.” Huu ni mwaliko wa kuishiriki
huruma kuu na upendo mkuu wa Mungu kwetu sisi wanadamu. Huruma hiyo na upendo huo
ndio unaotuwezesha kuyavuka maisha ya utu wa kale yaliyopita na kufanya bidii kuyazingatia
yale yaliyo mbele yetu (Rej. Fil 3:13).
Safari
ya maisha yetu, iliyo pia safari ya imani yetu, ni ndefu. Katika Agano la Kale, ililichukua
Taifa la Israeli miaka arobaini kuingia katika Nchi ya Ahadi. Kipindi kirefu ambacho,
pamoja na kutawaliwa na matendo makuu ya Mungu, kilitawaliwa pia na vishawishi vingi
hata kuwafanya Waisraeli wafikirie mara kadhaa kuiacha safari iliyowaelekeza mbele
kwenye Nchi ya Ahadi na kutamani kurudi nyuma, utumwani Misri. Kilikuwa kipindi kirefu
kilichojaa hisia mchanganyiko wa furaha na shukrani (Rej. Kut 15:1-21); kipindi pia
cha kutetereka kiimani na kukata tamaa kwa upande wa Waisraeli; hasa pale walipopata
shida (Kut 14:10-12; Hes 11:4-6). Lakini pia kilikuwa ni kipindi kirefu kilichodhihirisha
huruma na ustahimilivu wa Mungu; Mungu anayedumu kuwa mwaminifu kwa agano aliloweka
na watu wake.
Katika
Agano Jipya, ilimchukua Yesu siku arobaini za kufunga ambamo ndani yake Yesu anayeshiriki
hali yetu dhaifu, anatufundisha na kutuonesha njia ya kuvishinda vishawishi na dhambi.
Safari hii ya Yesu ya siku arobaini ilikuwa ni kielelezo cha kipindi cha maisha yetu;
maisha yanayoonja raha na karaha, yakidai kupokea yote hayo kwa jicho na uradhi wa
moyo unaoongozwa na imani. Ni kwa jicho tu la imani ndipo tunaweza kung’amua uzuri
wa mpango wa Mungu hata katika hali zile zisizofurahisha na kupendeza, kwani kwa njia
hiyo tunaweza kukaa chini na kutafakari tukitafuta kujua ni ujumbe gani Mungu anataka
kutufikishia kupitia matatizo na mateso yetu. Malezi haya ya kimungu mintarafu imani
ni kile tunachojifunza juu ya ukuu na adhama ya imani kama njia ya kwanza na ya msingi
kwa wokovu. Kujaribiwa kwake hakuna lengo jingine zaidi ya kuiimarisha na kuithibitisha.
Mtume Yakobo anatukumbusha kuwa, “kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi” (Yak 1:3;
Rej. 1Pet 1:7). Hivyo basi, ni matumaini yetu kuwa, pamoja na vikwazo na changamoto
nyingi tunazopitia katika safari ya imani yetu, kipindi cha Kwaresima kinatupatia
fursa ya mazoezi ya kiroho na tafakari zitakazotusaidia kukutana na Kristo Mfufuka.
SURA YA PILI
HALI HALISI YA IMANI Hali halisi ya
kiimani katika wakati wetu huu inadhihirisha ubaridi wa imani (indifference), kutokupendelea
mambo ya dini (agnosticism), mtazamo kwamba maoni binafsi ndiyo msingi na kipimo cha
maadili na maamuzi ya maisha binafsi (relativism), na pia kutukuza malimwengu (secularism).
Kipo pia kishawishi kikubwa cha kutaka kuugeuza ujumbe wa Injili kuonekana kuwa unafaa
tu kuwabidisha wakristo kujihusisha na harakati za kijamii, kisiasa na kiutamaduni
tu, bila yote haya kujengwa, kwa nafasi ya kwanza, juu ya imani kwa Kristo, aliye,
kwanza kabisa, Bwana na Mwokozi wa Roho zetu. Kadiri siku zinavyokwenda, angalizo
la Mwenyeheri Papa Yohane Paulo II linazidi kujidhihirisha wazi, kwani, “Vikundi vya
wabatizwa vimepoteza hamu na ladha ya imani… havijitambui tena kuwa wanakanisa, vikiishi
mbali na Kristo na mbali na Injili. Katika hali hiyo litatakiwa ‘tangazo jipya la
Injili’ au ‘marudio ya Injili’.”
Hali
hii sio tu kwamba imezikumba nchi zile zilizobahatika kuuishi ukristo kwa karne nyingi,
bali hata katika bara la Afrika, pamoja na kuonyesha dalili nyingi za kukua, bado
imani imeonesha dalili nyingi za kutetereka. Lipo tatizo kubwa la ushirikina hata
miongoni mwa wale wanaomwamini Kristo. Zipo sababu nyingi zinazochochea ushirikina.
Moja ya sababu hizo ni umasikini wa waamini unaowapelekea kukosa elimu, afya na maisha
bora. Mazingira kama haya yanafanya ushirikina ushamiri na kwa jinsi mtu anavyokuwa
dhaifu katika imani, vivyo hivyo anaathirika vibaya na upepo wowote utakaovuma. Kizazi
cha mtu aliye katika hali hii kinapokonywa fursa ya kurithishwa imani iliyo bora zaidi,
kwani mazingira yanayotawala yanakuwa ni ya kutafuta ufumbuzi wa matatizo kupitia
nguvu za giza, ambazo ndiyo huduma waliyonayo karibu, kuliko kupitia nguvu za mwanga,
kama elimu bora, afya bora na huduma za kiroho zilizo bora na karibu. Kundi la wale
wanaojitangaza kutomwamini Mungu, hasa kati ya wasomi walioathiriwa na ushawishi wa
kimagharibi, linazidi kukua pia. Zaidi sana ni kule kukosekana kwa malezi ya kina,
huu ukiwa ni udhaifu, kwa upande mmoja wa wachungaji wasiotenga muda wao wa kutosha
kwa ajili ya kutoa katekesi ya kina na endelevu kwa waamini, na kwa upande mwingine,
ugumu wa waamini kutoa muda wao kufuata mafundisho ambayo yangewajenga kiimani. Athari
ya malezi ya juu juu ya kiimani au ya watu kutopenda kufuata katekesi na mafunzo mengine
ni kubwa sana. “Leo katika Afrika ‘malezi ya kiimani… mara nyingi hukomea katika kiwango
cha chini sana, na dini nyingine kwa urahisi hunufaika katika ulegevu huu’.”
Siku hizi inakuwa vigumu sana
kumtofautisha mkristo na mtu mwingine yeyote asiye mkristo. Imekuwa dhahiri kwamba
wote wanatenda uovu uleule na kufuata mienendo ile ile mibaya inayoshusha utu na hadhi
ya mwanadamu. Udhaifu huu wa kushindwa kuiishi imani yetu kikamilifu unawafanya wakristo
washindwe kumpa Mungu utukufu na sifa kwa njia ya matendo yao. Mt. Ireneo anasema:
“Utukufu wa Mungu ni mwanadamu aliye hai kabisa.” Kwa maneno mengine, ndiyo kusema,
utukufu wa Mungu ni mwanadamu kuishi kikamilifu, kwa utauwa, akiyachukulia maisha
yake kuwa ni ushuhuda wa upendo wa Mungu duniani. Ukamilifu huu kwa mkristo unajidhihirisha
katika tendo la kuiweka imani katika matendo ya kila siku. Ukamilifu huu unawezekana
kwa sababu mkristo anamwamini Kristo aliyekuja ili ampatie uzima na awe nao tele;
yaani, awe nao katika ukamilifu wote (Rej. Yn 10:10). Na Kristo huyu ndiye ambaye
“ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu” (Yn 1:4). Kwa
hivi safari ya imani ndiyo inayotuvusha kutoka katika hali ya ilimradi naishi tu na
kuanza kuishi kikamilifu.
Mwaka
wa Imani kama ilivyokuwa kwa Sinodi ya 13 ya Kawaida ya Maaskofu iliyofanyika mwaka
uliopita (2012), ni mwaliko kwa wakristo kurudia kuchukua uamuzi madhubuti wa kuiishi
imani yao kikamilifu. Wakristo wanapaswa kutambua kuwa: “Bwana ndiye lengo la historia
ya kibinadamu, ‘kitovu cha matarajio ya historia na ya ustaarabu’, kiini cha uzao
wa kibinadamu, furaha ya kila moyo, na utimilifu wa matumaini yote.” Hili litadhihirika
kama Wakristo tutaupokea kwa moyo radhi wito wa Mtume Yakobo anayesema: “Iweni watendaji
wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu” (Yak 1:22). Kwa sababu,
“popote pale Mungu anapofungua mlango kwa neno ili kutangaza fumbo la Kristo (Rej.
Kol 4:3), papo hapo anapaswa kuhubiriwa kwa ujasiri (Rej. 1Kor 9:16; Rum 10:14) na
ushujaa mbele ya watu wote (Rej. Mdo 4:13. 29. 31…), Mungu aliye hai na Yule aliyemtuma
kwa ajili ya wokovu wa wote, yaani Yesu Kristo.”
SURA YA TATU
FUNDISHO
LA JUMLA
“Simameni imara katika imani” (1Kor 16:13). Hivi ndivyo Mtume
Paulo anavyowaandikia waamini wa Korintho. Anawahimiza wasimame imara katika imani
ili wasije wakapoteza zawadi hiyo kubwa iliyo mlango wa zawadi zote za kimungu. Kanisa
la Korintho lilikuwa limeanzishwa na Mtume Paulo mnamo mwaka 51. Baada ya kupanda
mbegu ya imani katika mji wa Korintho, Paulo alikaa hapo mwaka mmoja na miezi sita
(Mdo 18:11) akilijenga kanisa hili kwa mafundisho yake. Korintho ya wakati huo ilikuwa
tayari ni mji mkubwa, wenye watu wengi na mchanganyiko, watu waliokuwa na uwezo na
hadhi tofauti. Miaka mitano baada ya kuanzishwa kwa kanisa la Korintho, unajitokeza
mpasuko mkubwa unaotishia kutokomeza imani changa ya waamini wa Korintho. Tatizo la
kwanza lilikuwa ni mgawanyiko baina ya waamini walioanza kujiainisha kuwa ni wafuasi
wa mtume huyu au yule (Rej. 1Kor 1:12-15). Ulianza pia kujitokeza ulegevu katika kufuata
kanuni za ibada (1Kor 11:17-18); na utepetevu wa kimaadili (1Kor 1:12-15; 5:1-5; 6:12-20).
Msingi wa imani ulipotikiswa, wakristo wa Korintho walifikia hatua ya baadhi yao kuanza
kupinga ufufuko (1Kor 15:12). Katika hali hii ya upotofu ulioanza taratibu kuota mizizi.
Mtume Paulo anasimama kidete kuwakumbusha kuwa “kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri
kwetu ni bure na imani yenu ni bure” (1Kor 15:14). Mtume Paulo analihimiza Kanisa
lirudi katika njia ya misingi ya imani aliyokuwa amewafundisha. Anawaambia Wakristo
wa Korintho wakeshe na kusimama imara katika imani (Rej. 1Kor 16:13).
Matatizo na migogoro iliyokuwa inalikabili
Kanisa la Korinto ilitishia kuua imani changa ya waamini wa Korintho. “Kwa vipimo
vya kibinadamu hali ya Korintho haikuwa na rutuba nzuri kwa upandaji wa imani na maadili
ya kikristo, lakini kisichowezekana kwa akili ya binadamu, kiliwezekana kwa nguvu
ya Mungu.” Paulo anayatafutia ufumbuzi matatizo ya jumuiya hii akijengea yote juu
ya msingi wa imani.
Imani maana yake ni nini? Imani ni zawadi
tunayopata kutoka kwa Mungu. Zawadi hii inakuwa ndilo jina la uhusiano kati ya Mungu
na mwanadamu katika mpango wa ukombozi. Kwake yeye aliyepokea zawadi na jina hili,
imani inabeba maana yake halisi; yaani, imani, “ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo,
ni bayana ya mambo yasiyoonekana” (Ebr 11:1). Hii ni hali ya mwanadamu kuinua moyo
na akili yake kumwelekea Mungu na ahadi zake, kwa maana sisi tunaomwamini Mungu “twaenenda
kwa imani, si kwa kuona” (2Kor 5:7).
Haya
mambo “yatarajiwayo” na “yasiyoonekana” si nadharia isiyokuwa na msingi. Haya mambo
“yatarajiwayo” na “yasiyoonekana” ni tamanio la kuishi katika muungano na Mungu, Mungu
ambaye tumekwishamuona katika nafsi yake ya pili; yaani, katika Yesu Kristo. Kama
Yesu mwenyewe anavyosema, “Aliyeniona mimi amemwona Baba” (Yn 14:9), kwa sababu imani
“ni jibu la mtu kwa Mungu ambaye anajifunua mwenyewe na kujitoa mwenyewe kwa mwanadamu.”
Uhusiano huu mpya kati ya Mungu na mwanadamu ambao kwa njia ya Ubatizo, mwanadamu
anafanyika kuwa mwana wa Mungu, unatuwezesha kutembea katika imani ya yale tunayoyatarajia
katika ulimwengu ujao.
Neno
la Mungu na Sakramenti zake zinatufunulia njia za imani na zinakuwa ni hakikisho la
kile tunachokiamini. Na kama anavyosema Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, “Kwa kusadiki
na kujikabidhi kwa Mungu, tunaitikia neno la Mungu.” Mt. Ambrose anapowafundisha Wakristo
wapya waliobatizwa mabadiliko yanayoendana na Sakramenti ya ubatizo waliyoipokea anasema:
“Hapo awali mliona kwa macho ya mwili, sasa mnaona kwa macho ya moyo.” Hivi ndivyo
wale wote waliompokea Yesu kama Bwana na Mwokozi wao wanavyotakiwa kuishi na kutembea
kuelekea Ufalme wa Mungu. Kuona huku kwa macho ya moyo ndiyo kuona kwa imani. Hii
ndio kusema anayeamini ameamua kujikabidhi kwa Mungu na anaahidi kuishi kiaminifu
kadiri ya matakwa ya Neno la Mungu na ahadi zake. Tendo hili la imani kuu ya kusadiki
pasipo kuona (Rej. Yn 20:29) lina tuzo lake, kama anavyotusaidia kung’amua Mt. Agostino
anaposema: “Imani ni kuamini kile usichokiona, na tuzo ya imani hii ni kuona kile
ulichoamini.”
Imani
ndio inayotupatia hakikisho la msingi ambalo juu yake tunayasimika maisha yetu yote.
Imani inakuwa ni mlango usioweza kufungwa na yeyote. Kama tunavyosoma katika waraka
wa sita kati ya nyaraka saba zilizoelekezwa kwa makanisa, kanisa la Filadelfia wanaambiwa:
“Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga”
(Ufu 3:8). Mlango huu daima uko wazi na kwa neema ya Mungu kila mtu anaweza kuupitia,
iwapo tutakuwa tayari “kurekebisha maisha yetu kuendana na ukweli wa ulimwengu mpya.”
Kanisa katika Mwaka
huu wa imani linatuelekeza pia kukua katika imani kwa njia ya tafakari na kujifunza
kwa kina Kanuni ya Imani; yaani, imani tunayoikiri. Kwa njia ya Sakramenti; yaani,
imani tunayoiadhimisha. Kwa njia ya Amri Kumi za Mungu; yaani, imani tunayoiishi.
Na kwa njia ya tafakari ya Sala ya Bwana; yaani, imani tunayoisali. Hivi ndivyo mafundisho
ya Katekisimu ya Kanisa Katoliki yalivyopangwa na kubainisha kwa ufasaha mkubwa muhtasari
wa namna mkristo anavyotakiwa kuishi.
Imani kwa Mungu na kwa Neno
lake “Nasadiki kwa Mungu mmoja”. Msingi wa imani yetu ni Mungu katika Nafsi
Tatu; yaani, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Mungu anayetupatia zawadi ya imani anatutaka
tumtolee shukrani kwa kuiishi zawadi hii tukiwa tumeunganika naye katika Utatu wake
Mtakatifu. Katika Injili ya Yohane, Yesu alipowaasa wafuasi wake wasikitendee kazi
chakula kiharibikacho (Rej. Yn 6: 27) wao waliuliza wakitaka kujua wafanye nini basi:
“Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu?” (Yn 6:28). Hili ni swali ambalo tunaweza
kulifanya kuwa letu katika kipindi hiki cha Mwaka wa Imani, na bila shaka, katika
maisha yetu yote. Yesu anawajibu akisema: “Hii ndiyo kazi ya Mungu: mmwamini yeye
aliyetumwa na yeye” (Yn 6:29). Humo ndimo ulimo utimilifu wote wa mpango wa Mungu
anayejidhihirisha katika Utatu Mtakatifu. “Kukiri imani katika Utatu Mtakatifu – Baba,
Mwana na Roho Mtakatifu – ni kuamini katika Mungu mmoja ambaye ni Upendo (rej. 1 Yn
4:8): Baba, ambaye katika utimilifu wa wakati alimtuma Mwanae kwa ajili ya wokovu
wetu; Yesu Kristo, ambaye kwa fumbo la kifo chake na ufufuko aliukomboa ulimwengu;
Roho Mtakatifu, ambaye analiongoza Kanisa katika karne zote tunaposubiri ujio mtukufu
wa Bwana.”
Imani kwa Mungu inakuwa ni tendo linalotuinua kupitia
tendo la “utii wa imani”: “Utii wa imani lazima apewe Mungu anayejifunua (Rum 16:26;
taz. Rum 1:5; 2Kor 10:5-6). Kwa imani mwanadamu hujikabidhi kikamilifu na kwa uhuru
mikononi mwa Mungu, akitoa kwa Mungu mwenye kufunua “heshima kuu ya akili na utashi”,
na akikubali kwa hiari ufunuo anaopewa na Yeye. Ili imani hii iweze kutekelezwa, mtu
hana budi kutanguliwa na kusaidiwa na neema ya Mungu. Kadhalika hana budi kuwa na
msaada wa ndani wa Roho Mtakatifu anayesukuma moyo na kumwelekeza kwa Mungu, na anayefunua
macho ya akili na anayewapa “watu wote utamu katika kuukubali na kuuamini ukweli”.
Roho Mtakatifu huyohuyo hukamilisha imani daima, kwa njia ya mapaji yake ili ufunuo
ueleweke kwa undani zaidi.”
Neno la Mungu linabaki kuwa ni msaada
usiopimika unaotusaidia kung’amua kujifunua huku kwa Mungu. Imani yetu katika Kristo
hulishwa kwa neno la Kristo mwenyewe. “Imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia
huja kwa neno la Kristo” (Rum 10:17). Neno la Mungu linailisha imani yetu na kutupatia
hakikisho la kile tusichokiona na kukigusa sasa kupitia milango yetu mitano ya fahamu.
Imani inakuwa ni mlango wa sita wa fahamu ulio na umuhimu wa juu kwani inatusaidia
kutamani yale ambayo jicho halijapata kuona wala sikio kusikia (Rej. 1Kor 2:9). “Kwa
maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu”
(Rum 10:10).
Imani kwa Kanisa “Nasadiki kwa Kanisa moja, takatifu,
katoliki na la mitume”. Kanisa linabaki kuwa “Mama na Mwalimu” wa imani na ni chombo
cha kimungu kinachowaunganisha watu na Mungu na baina yao. Kwa sababu hiyo Mt. Ireneo
wa Lione anatukumbusha kuwa, “Lilipo Kanisa, yupo Roho wa Mungu: alipo Roho wa Mungu
lipo Kanisa na neema zote.” Kwa maneno mengine ndio kusema, lilipo Kanisa la kweli
lililoanzishwa na Kristo juu ya msingi wa Mitume hapo imani ya kweli ipo, kwa sababu,
“Kanisa la Mungu aliye hai”, ni “nguzo na msingi wa kweli” (1Tim 3:15). Hata hivyo,
ilipo imani hazikosekani changamoto. Kwa sababu, “hatusadiki tu kwa Kanisa, bali wakati
huo huo sisi nasi ni Kanisa.” Tunatambua wazi kwamba huku kuwa Kanisa ni safari ya
wongofu. Ni safari ya wongofu kwa kuwa ndani ya Kanisa wadhambi na watakatifu wanapata
nafasi, lakini wote wakialikwa kukua katika njia ya wongofu. “Kanisa … ambalo huwakumbatia
wakosefu ndani yake, na wakati uleule ni takatifu na linahitaji kutakaswa, haliachi
kamwe kutubu na kujitengeneza upya.”
Safari
yetu ya kukua katika imani ndani ya Kanisa inaifanya nafasi ya Kanisa kwa wokovu kuwa
ni ya muhimu sana. Umuhimu wake unatokana na ukweli kwamba lenyewe ni Mwili wa Fumbo
(Kol 1:18) wa Kichwa ambaye ni Kristo mwenyewe. Ndiyo maana, Kanisa “ni mwezi wa kweli.
Kutoka katika mwanga usiokuchwa wa nyota ya kidugu, linapata mwanga wa umilele na
wa neema. Kimsingi, Kanisa haliangazi mwanga ulio wake kwa asili, bali mwanga wa Kristo.
Kanisa linapata mng’ao wake kutoka kwenye jua la haki, ili baadaye liweze kusema:
mimi ninaishi, lakini si mimi bali Kristo anaishi ndani yangu (Gal 2:).” Ni kutokana
na uhusiano huu uliopo kati ya Kristo na Kanisa ndio maana Mt. Sipriano hasiti kutusaidia
kutambua kuwa; “Kama hatuna Kanisa kama mama, hatuwezi kuwa na Mungu kama Baba.”
Imani
iliyo hai Imani ambayo mwanzo wake ni Mungu mwenyewe, inapaswa kuwa hai na
kwa hulka yake, kila kilicho na uhai kinakua. Mitume walipoyasikia mafundisho ya Yesu
aliyeonya juu ya watu kuwa chanzo cha makwazo, Mitume wanaomba kuongezewa imani: “Bwana,
tuongezee imani” (Lk 17:5). Mahali pengine tunakutana ya Yesu anayemponya yule kijana
mwenye pepo. Pamoja na imani ya baba wa kijana huyu, bado alimwambia Yesu, “ukiweza
neno lolote, utuhurumie” (Mk 9:22). Yesu anamjibu akisema: “Yote yawezekana kwake
aaminiye” (Mk 9:23). Baba wa kijana anamalizia kwa kusema: “Naamini, nisaidie kutoamini
kwangu” (Mk 9:24). Haya yalikuwa baadhi ya matukio katika Injili ambayo yanatufunulia
ukweli kwamba, imani kwa asili yake inakua na inakua vema kama inakuzwa kwa msaada
wa neema ya Kristo.
Inapotokea kwamba kuna kutetereka katika
makuzi ya imani ni wajibu wetu kukumbushana na kuhimizana, ili tuweze kuamka na kusimama
tena katika imani. Huu ni mwaliko wa kurudi tena kwenye misingi ya imani na kujipima
ili kuona kama maisha yetu bado yamesimama katika msingi wa imani au tumeanza kupotoka.
Mtume Paulo akiwaandikia Wakorintho anawapa changamoto akisema: “Jijaribuni wenyewe
kwamba mmekua katika imani; jithibitisheni wenyewe. Au hamjijui wenyewe, kwamba Yesu
Kristo yu ndani yenu?” (2Kor 13:5). Mtume Paulo anawataka wajipime kuona ni kwa kiasi
gani na ni kwa namna gani waamini wa Korintho wamekua katika imani. Wakati kwa upande
mmoja imani hujaribiwa na Mungu, kwa upande mwingine Mtume Paulo anatushauri tujipe
nafasi za kujijaribu wenyewe ili tuone kama tunakua au tunadumaa katika imani. Zipo
namna nyingi za kujijaribu wenyewe katika imani, lakini njia ya uhakika kabisa ya
kujipima ni kuangalia ni kwa namna gani tunakua katika fadhila zile mbili zingine
za kimungu; yaani matumaini na mapendo.
Imani hai: dhihirisho la matumaini
na upendo Imani ya kweli inajidhihirisha katika matumaini na upendo. Fadhila
hizi tatu za kimungu haziachani (Rej. 1Kor 13:13). Upendo, kama anavyoandika Mt. Agostino,
kwa kawaida unatanguliwa na imani: “Upendo kwa Mungu na kwa jirani utatoka wapi bila
imani? Anawezaje mtu kumpenda Mungu asiyemwamini?” Imani ni ufunguo unaotuingiza katika
mji wa Mungu, mji ambao wale wanaoishi ndani yake, wanatembea kwa miguu ya matumaini
na upendo. Imani ya kweli ni lazima ijidhihirishe kwa kukua katika matendo ya upendo
(Rej. Yak 2:14-18 ). Huu ni ushuhuda wa upendo, unaojenga imani na kuikuza imani.
“Imani inakua pale inapotiwa katika maisha kama uzoefu wa upendo uliopokelewa na pale
inaposhirikishwa kwa wengine kama uzoefu wa neema na furaha. Inatufanya kuzaa matunda,
kwa sababu inapanua ndani ya mioyo yetu matumaini na kutuwezesha kuwa na ushuhuda
ulio hai: hakika, inafungua mioyo na akili za wale wanaosikiliza kuuitikia mwaliko
wa Bwana wa kushikilia neno lake wa kuwa wafuasi wake.” Imani pia inajenga matumaini
na matumaini ni dhihirisho la kile tunachokiamini. Kwa hiyo Mwaka wa Imani ni mwaliko
pia wa kukua katika fadhila hizi za kimungu.
Changamoto mbali mbali hasa
za mahusiano na watu wa Jumuiya nyingine za Kikristo na dini nyingine.
Kama
Wakristo Wakatoliki wa Tanzania tunaiishi imani yetu tukiwa katika jamii iliyo pia
na watu wenye imani tofauti na imani yetu. Kati ya hawa wapo wanaoamini baadhi ya
yale tunayoamini na wengine ambao hawaamini kabisa kile tunachokiamini. Pamoja na
tofauti zetu za kiimani, Kanisa Katoliki linaamini katika uhuru wa kuabudu na linaheshimu
watu wa dini na madhehebu yote. Kwa kuzingatia ukweli huo, Kanisa limejitahidi sana
kuunda mazingira ya mazungumzano kati yake na wakristo wa madhehebu mengine na watu
wa dini nyingine kwa lengo la kukuza mshikamano, kuheshimiana na kuelekeza nguvu zetu
katika kudumisha utu wa binadamu na amani ya Taifa letu.
Katika
siku za karibuni yamejitokeza matukio yasiyopendeza na ya kusikitisha. Kashfa dhidi
ya dini na madhehebu mengine zinazidi kuendelea na hali hiyo inaanza kuonekana kuwa
ni utamaduni usio rasmi wa Taifa letu kwa sababu unafumbiwa macho. Yamekuwepo matukio
ya kuchomwa moto kwa nyumba za ibada na baadhi ya vyombo vya habari vinavyomilikiwa
na madhehebu ya dini kutumika kuanzisha na kuendeleza malumbano, uchochezi, chokochoko
na kashfa za kidini. Hali hii haijengi na ni kukosa heshima kwa imani za wengine.
Kanisa linaamini kwa dhati kabisa kuwa, “Katika matumizi ya uhuru wowote, watu lazima
waheshimu kanuni ya kimaadili ya uwajibikaji wa binafsi na wa kijamii.” Kama Kanisa
Katoliki nchini tunawaomba waamini wetu msishawishike kutenda jambo lolote kinyume
na maelekezo ya upendo wa kiinjili. Kuweni macho mkidumu katika sala. Kuweni wapole
kama hua, lakini wenye busara kama nyoka (rej. Mt 10:16). Tunaomba msitumie muda wenu
kuhubiri juu ya imani zisizowahusu. Jikiteni katika kuijua na kuiishi imani yetu kwa
kina. Lakini pia tunaziomba mamlaka kuu kutoruhusu kujengeka utamaduni wa kusia mbegu
za chuki na migongano inayoteteresha imani. Tusikubali kufika mahali ambapo matukio
yasiyo ya kawaida yakaonekana kuwa ni ya kawaida, hasa yanapoendelea kutokea na nguvu
za dola zikaonekana kuwa kimya au kuzidiwa nguvu.
Ushuhuda wa Imani
Familia Imani
ya kweli inapimwa kupitia “afya” ya familia na ya jamii. Haya mawili yanategemeana.
Imani isipojidhihirisha katika uhai wa familia, iliyo Kanisa la kwanza, la nyumbani
na la msingi, itakuwa ni vigumu kujidhihirisha popote. Familia zetu zinazidi kuwa
legelege kwa sababu hazichukuliwi tena kuwa eneo la malezi muhimu ya kiimani na ya
kiutu. Malezi ya familia “yamebinafsishwa” katika tendo la kuamini kila mtu katika
familia ana wajibu wa kujilea mwenyewe bila ya msaada wa mwingine kati ya wale wanaounda
familia moja. Katika mazingira ya namna hii, dhana nzima ya familia inapotea na familia
inapoteza fursa ya kuwa “shule ya imani”, ambamo wazazi na watoto, kwa pamoja, wanakua
katika imani. Mwaliko huu wa Mtume Paulo kwa Kanisa la Korintho ni mwaliko kwanza
kwa hili “Kanisa la nyumbani”. Tunazihimiza familia zote za Kikristo kuizingatia imani
kwa dhati: Familia, “Simameni imara katika imani”! Ipelekeni nyumbani ile imani mliyoipokea
kutoka kwa Mungu kupitia Kanisa lake. Humo mkaiishi na kuijengea mazingira ya kukua.
Hili linapotekelezwa, familia itakuwa na uwezo wa kuipeleka imani katika jamii.
“Familia
inapata katika mpango wa Mungu Mwumbaji na Mkombozi sio tu utambulisho wake; yaani,
yenyewe ni nini, bali pia utume wake; yaani, ni nini inachoweza na inachopaswa kufanya”.
Familia zinapoutambua utambulisho wake na utume wake zinaweza kuiishi imani kwa namna
bora zaidi. Huo unakua ndiyo mwanzo wa ushuhuda wa kikristo. Ndani ya familia panakuwa
ni mahali unamozaliwa moyo wa huruma kwa wanyonge na wasiojiweza. Humo imani inakuwa
ni jibu la kutatua hali za kutoelewana katika familia. Ni kwa namna hii tunaweza kupiga
hatua ya kwanza katika kuboresha mazingira ya mahali tunamoishi, kwa sababu “familia
ni mahali panapofaa pa kujifunzia na kuzoeshwa utamaduni wa msamaha, amani na upatanisho”.
Kwa sababu hiyo wajibu wa malezi endelevu ya imani katika familia unapaswa kuwa wa
kudumu. Kwa namna hii tunaweza kuanza kupiga hatua ya kwanza katika kupambana na maradhi
hatari kama UKIMWI, kupambana na rushwa, uzembe, na tabia zote ambazo zina athari
mbaya kwa makuzi ya mtu binafsi na jamii kwa ujumla. Kwa njia ya imani familia zitapata
furaha ya kweli inayojengwa kupitia fadhila za amani na upendo.
Kazini
na katika Jumuiya Mwaliko wa kusimama imara katika imani hauishii kanisani
na katika familia tu, ila unaanzia hapo na kutoka hapo mwaliko huu unatekelezwa popote
tunapokwenda. “Kukiri kwa mdomo inaonesha kuwa imani inamaanisha ushuhuda na wajibu
wa hadharani pia. Mkristo hatakiwi kamwe kufikiri kuwa imani ni tendo la faragha.
Imani ni kuchagua kusimama na Bwana ili kuishi naye.” Kuipeleka imani katika jamii
ni tendo la ushuhuda wa kikristo. Mtume Yohane anatufundisha kuwa ni kwa njia ya imani
tu ndipo tunaweza kuushinda ulimwengu: “Na huku ndiko kuushinda ulimwengu: hiyo imani
yetu” (1Yoh 5:4). Tendo la ushuhuda wa mkristo linalojidhihirisha kwa njia ya imani
halina maana ya kujaribu kuwalazimisha watu wengine kuwa wakristo, bali ni kutia katika
matendo misingi ya upendo, haki, amani na maelewano kama Kristo anavyotuagiza, na
kwa namna hii tunatakatifuza maeneo ya kazi zetu za kila siku na jumuiya zetu. Huku
ndiko kuwa chumvi na nuru ya ulimwengu. Na Baba Mtakatifu Benedikto XVI anatuhimiza
akisema: “Hatuwezi kukubali chumvi ipoteze ladha au mwanga ubaki umefichwa (rej. Mt
5:13-16).”
Imani ya
kweli, ambayo inajidhihirisha katika tendo la waamini kujitoa kama vyombo safi ambavyo
Mungu anavitumia kuiumba upya na kuitakatifuza dunia, ni chachu ya kweli kwa mwanadamu
na kwa ulimwengu. “Je, si kazi ya Kanisa kutoa mwanga wa Kristo katika kila kipindi
cha historia? Si kazi yake kufanya uso wa Kristo ung’are pia mbele ya vizazi vya hii
milenia mpya?” Basi, wakati huu wa Kwaresima ni wakati wa kuifanya upya imani yetu
kwa njia ya Sakramenti za Kanisa, hasa Sakramenti ya Upatanisho. Vile vile, huu ni
wakati wa kufufua matendo ya huruma na upendo na kuyafanya kuwa endelevu katika maisha
yetu.
Kanisa hapa
nchini linatambua “mchango mkubwa ambao wanawake na wanaume walitoa na kusaidia kukua
na kuendelea kwa jumuiya kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao.” Baba Mtakatifu Mwenyeheri
Yohane Paulo II atabaki kwetu kuwa ni tunda la utakatifu uliojidhirisha katika uaminifu
wake kwa Kristo aliyemtanganza na kumtumikia. Maisha yake ya sala, uvumilivu, uongozi
wake shupavu na msimamo wake usiotetereka katika kuitafuta na kuikazia macho sura
ya Yesu, imemfanya kuwa shahidi wa imani anayepaswa kuwa mfano wa kuigwa. Wapo pia
Watanzania wenzetu ambao maisha yao yalikuwa ni kielelezo cha imani inayojidhihirisha
katika matendo. Mtumishi wa Mungu, Mwalimu Julius Nyerere, mwanasiasa mweledi, akiongozwa
na dhamiri ya kikristo, ni mmoja wa wakristo waliotukuka katika maisha ya uadilifu
wa kisiasa na kiutu. Mtumishi wa Mungu Sr. Bernadetta Mbawala wa shirika la masista
Wabenediktini wa Mt. Agnes Chipole, naye alifanikiwa kuitafsiri imani katika maisha
yake na hivi akaishi maisha ya upendo unaobubujika kutoka katika imani kwa Mungu na
kwa Kanisa. Wakumbukeni hawa na wengine wengi walioishi miongoni mwetu wakimshuhudia
Kristo kwa maisha yao, tena, “iigeni imani yao” (Ebr 13:7).
SURA
YA NNE
MATUKIO MUHIMU
Miaka 150 tangu Wamisionari wa Kwanza walipotua
visiwani Zanzibar Tunapotafakari mwaliko huu wa kusimama imara katika imani,
historia inatukumbusha pia kuwa miaka takribani 150 iliyopita, imani hii tunayoiishi
na kuiadhimisha ilitufikia kupitia visiwa vya Zanzibar. Yesu Kristo, aliye Mlango
wa Imani, ni Njia vilevile inayotuelekeza na kutuongoza kwenye Uzima. Yote huanzia
na kuishia kwake. Hata hivyo, Yeye aliye Njia na Mlango hutufungulia “njia” nyingine
nyingi na “milango” mingine mingi inayotuelekeza kwake Yeye aliye utimilifu wa yote.
Wamisionari wa Shirika la Roho
Mtakatifu walipofika Zanzibar, mnamo mwaka 1860, hawakuishia hapo, bali wakitokea
katika visiwa hivyo waliivusha mbegu ya imani hadi Tanganyika ya wakati huo na kuanza
kuipanda katika mji wa Bagamoyo mnamo mwaka 1868. Mbegu hii ya imani iliendelea kuchipuka
na kukua kupitia wamisionari wa mashirika mbali mbali; wakiwemo Wamisionari wa Afrika,
Wabenediktini wa Mt. Ottilia na wengine wengi baada yao, ambao wote katika ujumla
wao walikuja kwa lengo la kuinjilisha na kuhakikisha kuwa imani inaota mizizi yake
katika maeneo ya nchi yetu. Wamisionari hawa pamoja na kuwa na karama mbali mbali,
waliunganishwa na lengo moja ambalo lilikuwa ni kutangaza habari njema. Kwa sababu
hiyo, kila kundi, kwa wakati wake na kwa namna yake limetoa mchango wake uliotukuka,
ama katika kupanda au katika kumwagilia mbegu na mche wa imani, na Mungu ameendelea
kuukuza huu mche wa Imani (Rej. 1Kor 3:6).
Kumbukumbu hii
inapaswa kuijaza mioyo yetu shukrani kwa Mungu aliyetupatia zawadi ya imani, zawadi
iliyo kuu ya upendo wake. Shukrani yetu inapaswa, hata hivyo, kuvuka mipaka ya kubaki
katika maneno tu na kuwa tendo la kudumu kiaminifu katika imani, kuifanya imani kuwa
dira inayoongoza kila tendo la maisha yetu ya kila siku na kuhakikisha kuwa imani
tuliyoipokea inazidi kustawi na kushamiri.
Mwaka wa Imani na Mkutano wa
Kawaida wa Kumi na Tatu wa Sinodi ya Maaskofu
Mwezi Oktoba 2012, kuanzia
tarehe 7 hadi 28, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alikutana Roma na Maaskofu kutoka ulimwenguni
kote kwa ajili ya Sinodi ya 13 ya Kawaida ya Maaskofu iliyokuwa na mada: “Uinjlishaji
Mpya kwa ajili ya Kueneza Imani ya Kikristo”. Sinodi hii ilikuwa na lengo la kuzindua
programu ya Uinjlishaji Mpya. Sinodi ilitafakari kwa kina njia mpya na muafaka zitakazolisaidia
Kanisa na wanakanisa wote kuifanya imani kuwa ni sehemu ya uhalisia wa maisha ya kila
siku ya waamini, kwa kuiishi kwa ari inayokuwa na kukomaa katika maneno, matendo na
mienendo ya maisha.
Tarehe 11 Oktoba 2012, Baba Mtakatifu Benedikto
XVI alizindua Mwaka wa Imani ambao utafikia kilele chake wakati wa maadhimisho ya
Sherehe ya Kristo Mfalme tarehe 24 Novemba 2013. Lengo msingi la Mwaka wa Imani
limewekwa bayana na Baba Mtakatifu katika hati yake Porta Fidei (Mlango wa Imani).
Mwaka wa Imani ni mwaliko wa
kurudia upya ungamo la imani na kulitia katika matendo ya maisha ya kila siku. Ni
wakati wa kupokea kwa shukrani zawadi ya imani ambayo kwa ubatizo mlango wa mahusiano
ya kina na Mungu unafunguliwa. “‘Mlango wa Imani’ (Mdo 14:27) daima umefunguliwa kwa
ajili yetu na kutuongoza katika muungano na Mungu na kutuingiza ndani ya Kanisa lake.
Inawezekana kuvuka kizingiti hicho pale neno la Mungu linapotangazwa na moyo unapojiruhusu
kuundwa kwa kugeuzwa na neema. Kupita katika mlango huo ni kuanza safari itakayodumu
kwa maisha yote.” Safari hii kwa wakati wa sasa inabeba pia mwaliko wa Uinjilishaji
Mpya kwa sababu zipo dalili na maelekeo makubwa ya Wakristo kusahau au/na kuzembea
maisha ya imani.
Imani
ya Kanisa sio tu matamko mbalimbali ya Kanisa, bali ni uhusiano hai na Yesu Kristo,
aliye Kichwa cha Kanisa, na uhusiano na Mwili wake, yaani Kanisa. Tunachokiamini ni
Ukweli uliofunuliwa kwetu na Yule ambaye ndani yake tunaamini, Yesu Kristo, Ukweli
unaoendelezwa na Kanisa chini ya maongozi ya Roho Mtakatifu. Kwa hivi, Kanisa lina
wajibu huo wa kuiendeleza imani kwa kuwa, “Kazi ya kueneza Injili ni wajibu na ndio
utume halisi wa Kanisa.”Njia ya kutekeleza wajibu huo ni “kutweka mpaka kilindini”,
ambako ndiko dhamana ya wakati huu wa kihistoria kwa Kanisa iliko. Hatua hii ya matumaini
italiwezesha Kanisa kuchukua hatua mpya mbele katika historia.
SURA
YA TANO
IMANI KATIKA MAISHA YA KISIASA
Tunapoisoma Barua kwa Dionyeto,
moja ya barua za kikristo za karne ya pili, tunaambiwa ifuatavyo juu ya wakristo wa
Kanisa la mwanzo: “Wanashiriki kila jambo kama raia… Wanatii sheria zilizowekwa na
maisha yao ya uadilifu wanayaishi vizuri kupita madai ya sheria.” Anaendelea kusema
pia, “kama roho ilivyo kwa mwili ndivyo wakristo walivyo kwa dunia.” Ushiriki wa waamini
katika shughuli za jamii na siasa ni sehemu ya wajibu wa kiimani. Lengo la ushiriki
huu ni kusaidia kujenga jamii iliyo bora zaidi, kwa sababu, “ili kuunda maisha ya
kisiasa yaliyo kweli ya kibinadamu, hakuna lililo bora zaidi kuliko kustawisha ndani
ya watu hisia za haki, upendo na huduma kwa manufaa ya wote.” Kwa kutekeleza wajibu
huu wakristo wanapata fursa ya kuwa “mwanga na nuru” kwa ulimwengu (Mt 5:14) na kuwa
“wahudumu wa hekima ya kikristo” katika jamii inayowazunguka.
Katiba
ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania
Taifa letu lipo katika kipindi mahsusi
cha historia. Katiba yetu inaandikwa upya. Uamuzi huu ni matokeo ya tafakari ya kina
iliyobaini kuwa kuna uhitaji wa sisi kama taifa kuwa na Katiba inayokwenda na wakati
na zaidi sana Katiba itakayotoa dira ya taifa kwa kipindi kirefu kijacho. Tunapenda
kuwaalika wakristo wote na watu wote wenye mapenzi mema kutekeleza zoezi hili kwa
umakini na uadilifu mkubwa, tukitambua kuwa suala hili la Katiba ni wajibu uliotukuka
ambao raia wanaushiriki katika maisha yao. Wakati dini, makabila na hali zetu zinatutofautisha,
Katiba ya nchi inabaki kuwa ni chombo kinachotuunganisha katika kuwa na haki sawa
na wajibu sawa, ndani ya nchi yetu. Imani zetu hazitunyang’anyi na wala hazilengi
kutufanya kupoteza utaifa wetu bali zinatusaidia kuijenga misingi ya mshikamano, amani
na uadilifu ambayo dini zetu zinapaswa kutufundisha kuitekeleza.
Wajibu
huu kwetu ni mkubwa kwa sababu tunapoutekeleza tunachangia kujenga misingi imara ya
Taifa, nalo ni jambo lililo muhimu sana. Mzaburi anatukumbusha anapouliza: “Kama misingi
ikiharibiwa mtu mwadilifu atafanya nini?” (Zab 11:3). Misingi yoyote ile, iwe ya imani
au ya Taifa inapoharibiwa hata mtu mwadilifu anatetereka. Fursa kama hii ya kuipitia
upya Katiba inakuwa ni wajibu wenye msukumo wa dhamiri kutoa mchango wetu ili hatimaye
tuwe na Katiba bora. Katiba isiyoheshimiwa inaporwa uhai wake. Tungependa kuona sisi
tulio Wakristo, tunaosukumwa na Amri Kuu ya upendo, kwa Mungu na kwa jirani (Rej.
Mt 22:36-40), tuwe msitari wa mbele katika kuheshimu sheria, taratibu na kanuni za
nchi zinazotuongoza.
Zoezi la kutoa maoni ya Katiba lina hatua
mbalimbali. Tume imekwishaanza kazi yake. Tunapoendelea na zoezi hili ni vema “tujiulize
kama tunaamini kweli Mafundisho ya Mungu na tuko tayari kuwajibika mbele ya Mungu
na mbele ya jamii juu ya maamuzi na vipaumbele vyetu? Je, tunaamini kweli ujumbe wa
Kristo kuwa Mungu ni Baba wa watu wote ambao huunda familia ya wanadamu?” Ni kwa sababu
hiyo, tunapendekeza Katiba yetu itamke wazi kuwa hakuna mtu yeyote aliye juu ya Katiba.
Iwe ni Katiba inayoweza kumhoji kila mtu, wakati wowote na aliye katika nafasi yoyote.
Iwe ni Katiba inayolinda na kutetea uhai na hadhi ya mtu tangu kutungwa mimba mpaka
kufa kifo cha kawaida. Katiba itamke wazi pia juu ya familia inayoundwa na baba, mama
na watoto. Zaidi sana, tungependa Katiba ifufue roho halisi ya uraia, yaani uzalendo
wa kitanzania. Katiba isipotafsirika kama dhamiri ya wajibu wa kizalendo itakuwa imeporwa
uhai wake. Katiba iwe zao la uadilifu na ikabidhiwe kwa utekelezaji wake kwa wale
ambao, si zaidi kwa maneno bali kwa matendo, wanajipambanua kuwa waadilifu kwa kila
hali. Katiba itakosa “uhai” wake kama wale waliopewa wajibu wa kuilinda, kuitetea
na kuisimamia hawafanyi hivyo.
Lakini ikumbukwe wazi kwamba wajibu
wa kuilinda na kuitetea Katiba, kwa nafasi ya kwanza, ni wajibu wa kila raia. Katiba
ni mali ya wananchi. Wale waliopewa dhamana ya kuilinda na kuisimamia si wamiliki
wa Katiba bali mawakili tu wanaopaswa kukumbuka siku zote kuwa wameajiriwa na wananchi
kuisimamia Katiba na si kuitawala Katiba.
Hatuna budi kutafakari
na kujiuliza ni kwa nini, pamoja na kuwa na Katiba na sheria unaendelea kutawala utamaduni
wa “kujichukulia sheria mkononi” iwe ni kwa wananchi wa kawaida na hata kwa wale waliopewa
dhamana ya kuilinda, kuitetea na kuisimamia Katiba. Raia wanapojichukulia sheria mkononi
ni dhihirisho la kutokuwa na imani na wale waliopewa dhamana ya kuisimamia sheria.
Na pale inapotokea wale waliopewa dhamana ya kuilinda na kuitetea wanajichukulia sheria
mkononi kwa kuipindisha, kwa kutoitetea na kuilinda hilo ni dhihirisho la kutokuamini
kwa dhati kile walichotamka mbele ya Mungu na wananchi. Tunarudia kusema kwamba, tunapaswa
kuunda na kujenga utamaduni wa kuheshimu Katiba, sheria na taratibu zinazotuongoza.
HITIMISHO Tunapenda kuhitimisha ujumbe huu wa Kwaresima
ya mwaka huu tukizidi kuwatia moyo wa kudumu imara katika safari ya imani, “tukimtazama
Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu” (Ebr 12:2). Tusikubali kupoteza
imani yetu. Hata pale mwendo katika safari ya imani unapogeuka kuwa mgumu, simameni
imara “mkidumu tu katika ile imani, hali mmewekwa juu ya msingi, mkawa imara; msipogeuzwa
na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake” (Kol 1:23).
Kipindi cha Kwaresima, kama ulivyo pia
Mwaka wa Imani, ni safari kuuelekea Ufufuko wa Bwana, ambao ni mlango wetu sisi wa
kuingia katika maisha mapya ya uzima wa milele. Kumshuhudia Kristo Mfufuka ni kuishi
katika upya wa maisha. Na kwa kuwa tunazidi kupoteza tunu bora za kuishi katika upya
wa maisha, hatuna budi kujikita katika Uinjilishaji Mpya wenye lengo la kutufanya
upya katika wajibu wetu wa Kikristo na kusaidia kuufanya ulimwengu kuwa mahali ambapo
Mungu anapewa utukufu na sifa. Tunawaalika pia kushiriki kikamilifu kalenda na mipango
iliyopendekezwa na Kanisa la Ulimwengu kwa Baraza la Maaskofu, Majimbo, Parokia, Vigango
na Vyama vya Kitume. Msiogope. Hatuko peke yetu. Simameni imara katika imani. Pamoja
nasi katika safari hii ya imani tunaye Mama Mbarikiwa Bikira Maria. Huyu ni Mama wa
Imani, aliyepata heri kwa sababu alisadiki na kwa kusadiki kwake yakatimizwa aliyoambiwa
na Bwana (Rej. Lk 1:45). Tunawatakieni safari njema ya imani katika mfungo wenu wa
Kwaresima. Safari hii imfikishe kila mmoja wetu kwenye furaha ya Pasaka ya Ufufuko.
Ni sisi Maaskofu wenu, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Dar es Salaam Mhashamu
Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Iringa Mhashamu Askofu Mkuu Norbert Mtega, Songea Mhashamu
Askofu Mkuu Josaphat Lebulu, Arusha Mhashamu Askofu Mkuu Paul Ruzoka, Tabora Mhashamu
Askofu Mkuu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi – Mwanza Mhashamu Askofu Telesphor Mkude,
Morogoro Mhashamu Askofu Gabriel Mmole, Mtwara Mhashamu Askofu Bruno Ngonyani,
Lindi Mhashamu Askofu Anthony Banzi, Tanga Mhashamu Askofu Agapiti Ndorobo,
Mahenge Mhashamu Askofu Evaristo Chengula, IMC, Mbeya Mhashamu Askofu Augustino
Shao, CSSp, Zanzibar Mhashamu Askofu Damian Kyaruzi, Sumbawanga Mhashamu Askofu
Severine NiweMugizi, Rulenge-Ngara Mhashamu Askofu Desiderius Rwoma, Bukoba Mhashamu
Askofu Method Kilaini, Bukoba Mhashamu Askofu Damian Dallu, Geita Mhashamu
Askofu Ludovick Minde, ALCP/OSS, Kahama Mhashamu Askofu Alfred Leonard Maluma,
Njombe Mhashamu Askofu Castor Paul Msemwa, Tunduru-Masasi Mhashamu Askofu Beatus
Kinyaiya, Ofm Cap, Mbulu Mhashamu Askofu Michael Msonganzila, Musoma Mhashamu
Askofu Isaack Amani, Moshi Mhashamu Askofu Almachius Rweyongeza, Kayanga Mhashamu
Askofu Rogath Kimaryo, CSSp,Same Mhashamu Askofu Salutaris Libena, Ifakara Mhashamu
Askofu Eusebius Nzigilwa, Dar es Salaam Mhashamu Askofu Renatus Nkwande, Bunda
Mhashamu Askofu Gervas Nyaisonga – Dodoma Mhashamu Askofu Bernadin Mfumbusa – Kondoa Mhashamu
Askofu John Ndimbo - Mbinga