Mikutano ya Makardinali ni fursa ya kusali, kutafakari na kushirikishana mang'amuzi
na vipaumbele vya Kanisa
Makardinali wanaendelea kusali, kutafakari na kushirikishana mang'amuzi, matatizo,
changamoto, fursa za vipaumbele kwa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu
ya Ukristo, wakati huu wanapojiandaa kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro, baada ya
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kung'atuka kutoka madarakani na sasa anaendelea
kulisindikiza Kanisa kwa njia ya sala na tafakari ya kina.
Historia ya Kanisa
inaonesha kwamba, Kardinali Walter Kasper, aliyetimiza miaka 80 tangu alipozaliwa
mapema juma hili, ataendelea kuwamo kwenye orodha ya Makardinali wenye haki ya kupiga
na kupigiwa kura na kwamba, ndiye Kardinali mwenye umri mkubwa kupita wote aliyebahatika
kupata dhamana hii katika mchakato wa kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hii inatokana
na ufafanuzi wa kisheria uliotolewa kwamba, haki ya Kardinali kupiga au kupigiwa kura
kutokana na umri unaanza pale kiti cha ukulu wa Mtakatifu Petro kinapokuwa wazi.
Makardinali
wanaendelea kuchambua kwa kina na mapana kuhusu changamoto zilizobainishwa na Mababa
wa Sinodi ya Maaskofu kuhusu dhamana ya Uinjilishaji Mpya, Kanisa na Ulimwengu, uhusiano
kati ya Mabaraza ya Kipapa na Maaskofu, bila kusahau matarajio ya Makardinali kuhusu
wasifu wa Papa Mpya, atakayeliwezesha Kanisa kuendeleza na kudumisha utawala bora.
Padre
Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Makardinali waliotoka
Marekani walikuwa wamejiwekea utaratibu wa kukutana na kubadilishana mawazo na Waandishi
wa Habari kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanalofuatilia mchakato wa uchaguzi wa
Papa Mpya hapa Vatican kwamba, utaratibu huo kwa sasa umefutwa.
Anakumbusha
kwamba, mikutano ya Makardinali inayoendelea kwa sasa si Sinodi wala Makongamano ambayo
viongozi wa Kanisa wanaweza kushirikisha mawazo na maoni yao au yale yaliyojiri katika
mikutano hiyo! Mikutano ya Makardinali kwa sasa ni fursa ya kusali, kutafakari na
kupembua vipaumbele vya Kanisa, ili hatimaye, kuwawezesha Makardinali kufanya maamuzi
ya busara wakiongozwa na Roho Mtakatifu, kwa ajili ya mafao na maendeleo ya Kanisa
la Kristo.
Hii ni mikutano ya faragha anasema Padre Federico Lombardi, ili
kutoa fursa kwa Makardinali kuwa huru kushirikisha mawazo yao kwa Makardinali wengine.
Waamini na watu wenye mapenzi mema, wanaalikwa kwa namna ya pekee kuvuta subira, kuhusu
tarehe ya kuanza uchaguzi wa Papa Mpya. Kwa sasa mwelekeo ni kwamba, Makardinali wanataka
kupata nafasi pana zaidi kwa ajili ya kusali, kutafakari na kupembua hali ya maisha
na utume wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo unaogubikwa na changamoto nyingi. Kutokana
na mantiki hii, hakuna haraka ya kupanga tarehe kwa sasa, lakini wakati ukiwadia waamini
watajulishwa.
Padre Federico Lombardi anasema kwamba, Pete ya Mvuvi iliyokuwa
inatumiwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita wakati wa uongozi wake kama
Khalifa wa Mtakatifu Petro, imekwaruzwa na haiwezi tena kutumika na kwamba, itahifadhiwa.