2013-03-07 12:46:18

Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Kimataifa, tarehe 8 Machi 2013


Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, inayofanyika kila mwaka ifikapo tarehe 8 Machi ni fursa ya kufanya tafakari ya kina ili kuangalia matukio yanayopelekea unyanyasaji na dhuluma dhidi ya wanawake, ili kuibua mbinu mkakati wa kuwa na kesho iliyo bora zaidi kwa wanawake wengi zaidi. Kuna wanawake wanaoendelea kunyanyasika kiasi hata cha kuamua kutema zawadi ya uhai ili kuficha aibu yao.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon katika ujumbe wake kwa Siku ya Wanawake Duniani inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 8 Machi, anawaalika watu kuondokana na mambo yanayopelekea nyanyaso na dhuluma kwa wanawake, kwa kujali na kuthamini utu na heshima yao; wahusika wakamatwe na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria, ili kukomesha tabia hii inayoendelea kukua na kupanuka katika Jamii nyingi.

Katika maeneo ambayo kuna vita na migogoro ya kivita, unyanyasaji wa kijinsia umekuwa ni silaha nyingine inayotumiwa na wanajeshi ili kuwadhalilisha maadui, lakini wanashindwa kutambua kwamba, wanadhalilisha utu na heshima ya mtu. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anapenda kuwahakikishia wanawake wanaoteseka, wanaodhulumiwa na kunyanyasika kwamba, Jumuiya ya Kimataifa iko pamoja nao.

Umoja wa Mataifa unataka kuwasaidia kwa kutoa kipaumbele cha pekee katika kupinga udhalilishaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na kwamba, wanawake watambuliwe na kuheshimiwa kama wadau wakuu wa ujenzi wa amani katika Jamii. Ikumbukwe kwamba, wanawake wanayo haki ya kuishi bila kunyanyasika.







All the contents on this site are copyrighted ©.