2013-03-07 12:10:23

Boresheni hali ya wanawake katika nchi zinazoendelea ili wachangie katika sekta ya maendeleo!


Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Kimataifa inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 8 Machi, Umoja wa Mataifa unaendelea kuzihamasisha Serikali na wadau mbali mbali kuongeza juhudi katika kuwajengea uwezo wanawake kwa njia ya elimu ili kupambana na changamoto mbali mbali wanazokabiliana nazo katika maisha yao ya kila siku. Juhudi hizi hazina budi kwenda sambamba pia na harakati za kupambana na umaskini, njaa na lishe duni.

Haya yamo kwenye taarifa ya haki msingi za binadamu iliyotolewa hivi karibuni na Baraza la Haki Msingi za Binadamu la Umoja wa Mataifa. Shughuli za uzalishaji katika sekta ya kilimo hasa kwa ajili ya chakula cha kifamilia inafanywa kwa sehemu kubwa na wanawake, kwani wanaume wengi wako mijini wakitafuta fursa za ajira. Licha ya ukweli kwamba, wanawake ndio wazalishaji wakuu katika sekta ya kilimo, lakini bado wanatumia nyenzo duni na wengi wao hawana elimu ya kutosha kuongeza tija na uzalishaji.

Kuna haja pia kwa Serikali kufanya maboresho katika sheria kandamizi dhidi ya wanawake pamoja na kutoa huduma za msingi kwa wanawake na familia zao. Wanawake wanahitaji kupata maji safi na salama, nishati ya uhakika, huduma bora za afya na elimu kwa ajili yao wenyewe na watoto wao. Baraza la Haki Msingi za Binadamu la Umoja wa Mataifa linasema kwamba, wanawake wakiwezeshwa kikamilifu wanaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa uzalishaji katika sekta ya kilimo na mapambano dhidi ya baa la njaa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.