2013-03-06 12:32:12

Makardinali wanasema, ndani ya Kanisa hakuna haraka ya uchaguzi!


Kardinali Antonio Maria VegliĆ² anasema, Makardinali hawana haraka ya kukimbilia kufanya uchaguzi wa Papa Mpya, bado wanapenda kutumia fursa hii ili kusali, kutafakari pamoja na kujadili kuhusu hali ya maisha na utume wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, matatizo, fursa na changamoto zilizopo, ili kuweza kujipanga vizuri zaidi.

Makardinali waliotoka nje ya Roma wanapenda kufahamu kwa undani zaidi kashfa zilizojitokeza kwa kuvujisha siri za Vatican, kwa kile ambacho kwa wengi sasa kinajulikana kama "Vatileak.". Hii ni haki na wajibu wao kwani wao ni viongozi waandamizi wa Kanisa.

Kutokana na changamoto mbali mbali zinazoendelea kulikabili Kanisa kwa sasa, Kanisa linahitaji kuwa na Baba Mtakatifu mwenye utakatifu wa maisha, ili uweze kuwa ni mfano na kielelezo cha kuigwa na wengine; awe ni mtu mwenye hekima na busara, fadhila zitakazomsaidia kutekeleza maamuzi yake msingi katika wajibu wa: kufundisha, kutakatifuza na kuwaongoza watu wa Mungu.

Ikiwezekana awe na umri utakaomwezesha pia kukabiliana na changamoto za safari na maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro; akiwa na afya njema, ni sifa ya ziada, lakini yote haya Makardinali wanamwachia Roho Mtakatifu ili awasaidie na kuwaongoza katika uchaguzi wa Papa Mpya.

Ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia sanjari na mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, yanahitaji kiongozi ambaye atakuwa mkweli na shahidi wa uinjilishaji Mpya ili kwa njia ya ushuhuda wa maneno na matendo yake, aweze pia kukabiliana na changamoto za maadili yanayotokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia katika tiba na afya ya mwanadamu.

Mahali anapotoka mtu kijiografia si tatizo la Kanisa, wala Makardinali hawaangalii rangi ya mtu haya ni matatizo yanayopigiwa debe na vyombo vya habari kwa masilahi yao binafsi. Makardinali wanasema, hakuna haraka ya kufanya haraka ya uchaguzi wa Papa Mpya, kwani wanataka kufanya upembuzi wa kina kuhusu maisha na utume wa Kanisa, ili kutoa dira na mwelekeo sahihi kwa Kanisa kwa siku za usoni, ili kujenga umoja, upendo na mshikamano kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.