Katiba ya nchi inapaswa kuheshimiwa na wote kwani ni mhimili wa umoja na mshikamano
wa kitaifa!
Baraza la Maaskofu Katoliki Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Congo limemwandikia
barua Rais Joseph Kabila wa DRC kwa kusisitiza kwamba, kwa vile Katiba ya nchi ni
sheria mama inapaswa kulindwa na kuheshimiwa na wananchi wote wa DRC bila ubaguzi
kwani hii ni nguzo muhimu ya umoja na mshikamano wa kitaifa.
Hivi karibuni,
serikali iliamua kufanya marekebisho kwenye Ibara ya 220 ya Katiba ya nchi, jambo
ambalo linapingwa na Baraza la Maaskofu Katoliki DRC. Maaskofu wanasema, Ibara hii
ni muhimu sana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa DRC, kumbe kuna haja
kwa wananchi kufahamu vyema Katiba, ili kuisimamia, kuilinda na kuitekeleza.
Maaskofu
Katoliki DRC katika barua yao kwa Rais Kabila wamegusia pia hali ya kisiasa, kiuchumi
na maendeleo ya kijamii. Wanampongeza kwa kuanzisha mchakato wa majadiliano ya kisiasa
yanayopania kuleta amani na utulivu kutokana na kinzani zilizojitokeza wakati wa kutangaza
matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika nchini DRC, hapo Novemba 2011.
Kuhusu
masuala ya uchumi na maendeleo Maaskofu wanabainisha kwamba, kuna matumizi mabaya
ya rasilimali ya nchi, kwani wanaofaidika ni watu wachache wakati mamillioni ya wananchi
wa DRC bado wanaendelea kuogelea katika dimbwi la ujinga, umaskini na maradhi. Ukata
na hali ngumu ya maisha ya wananchi wa DRC unawatia uchungu kama viongozi wa kidini.
Kuna haja ya kubadilisha mwelekeo huu ili rasilimali ya nchi iweze kuwa ni kwa ajili
ya mafao ya wengi.
Ili kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu, Maaskofu
Katoliki DRC wanasema, kuna haja ya kufanya mabadiliko makubwa katika mfumo wa mahakama
na kwenye vikosi vya ulinzi na usalama. Umefika wakati muafaka kwa Serikali na wananchi
kwa ujumla kusimama kidete kupambana kufa na kupona na rushwa na ufisadi. Serikali
ianzishe mikakati itakayowezesha amani na utulivu kutawala tena eneo la Mashariki
ya DRC, ambalo wananchi wake wanaishi kwa hofu na vitisho kutokana na uwepo wa makundi
yenye silaha.