Vitendo vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu!
Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria linasema kwamba, waamini na watu wote wenye mapenzi
mema, wanachangamotishwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu
na jambo lolote linalokwenda kinyume cha utu wa mwanadamu linapingana na mpango wa
Mungu. Maaskofu wameyasema hayo mara baada ya kuhitimisha Kongamano la Kimataifa lililokuwa
linajadili pamoja na mambo mengine kuhusu "imani na utu wa binadamu".
Baraza
la Maaskofu Katoliki Nigeria linabainisha kwamba, makosa yanayodhalilisha utu na heshima
ya binadamu ni pamoja na: mauaji, utoaji mimba, kifo laini, kujinyonga, ukeketaji,
mauaji ya kimbari, madhulumu, maisha duni, vifungo vya watu wasiokuwa na hatia, utumwa,
ukahaba, biashara haramu ya binadamu pamoja na hali na mazingira duni ya kazi.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Nigeria linasema kwamba, nchini mwao wanakabiliwa na mambo yanayohatarisha
utu na heshima ya binadamu. Mambo haya ni pamoja na ukosefu wa utawala bora; ukosefu
wa ulinzi na usalama; rushwa na ufisadi; mmong'onyoko wa maadili na kanuni bora za
uongozi; udhalilishaji wa haki msingi za raia wa Nigeria kwa misingi ya kikabila,
kidini, kijinsia na kijiografia na mahali anapotoka mtu.
Haya ni baadhi ya
mambo yanayohatarisha na kuendelea kunyanyasa utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu. Vitendo vya kigaidi vinavyotekelezwa na kikundi cha Boko
Haram na makundi yenye silaha ni hatari kwa heshima na utu wa mwanadamu. Baraza la
Maaskofu Katoliki Nigeria lina laani mauaji yanayofanywa kwa misingi ya kidini; nchi
ambayo kwa sasa uhuru wa kuabudu uko mashakani na unatolewa kwa baadhi ya wananchi
tu jambo ambalo kamwe haliwezi kukubalika!