2013-03-02 14:48:51

Pete ya mvuvi iliyotumiwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kuhifadhiwa!


Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, ukarabati wa Kikanisa cha Sistina kitakachotumika kwa ajili ya mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya bado haujaanza na kwamba, kwa sasa inatakiwa idhini kutoka kwa mkutano wa Makardinali unaoanza kikao chake cha kwanza, Jumatatu, tarehe 4 Machi 2013, asubuhi.

Chumba cha kitume kilichokuwa kinatumiwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro, kwa sasa kimefungwa rasmi baada ya kukamilisha taratibu zote kadiri ya sheria za Kanisa. Ile Pete ya Mvuvi iliyokuwa inatumiwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita wakati wa uongozi wake haitavunjwa na badala yake itahifadhiwa kwenye Msalaba, kiasi kwamba haitaweza kutumiwa tena, kama walivyofanya kwa Pete ya Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, ambayo kwa sasa imehifadhiwa pia kwenye kioo maalum.

Padre Lombardi amefafanua kwamba, kuna Makardinali 75 wanaoishi na kutekeleza utume wao hapa mjini Roma. Makardinali 66 hadi kufikia Jumamosi walikuwa wamekwisha wasili mjini Roma na tayari wamekwisha wasiliana na Dekano wa Makardinali Angelo Sodano. Baadhi ya Makardinali wasiokuwa na haki ya kupiga wala kupigiwa kura wameonesha nia ya kutoshiriki katika mkutano wa Dekania ya Makardinali hasa kutokana na sababu za kiafya na uzee.

Kila siku jioni katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, waamini watasali Kanuni ya Imani pamoja na Sala maalum zilizotayarishwa kwa ajili ya kuwaombea Makardinali wakati huu wanaposhiriki katika mchakato wa kumchagua Papa Mpya.







All the contents on this site are copyrighted ©.