2013-03-02 11:09:32

Mshikamano katika matumaini!


Uongozi wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika kipindi cha miaka minane, umeacha chapa ya kudumu katika mioyo ya watu wengi. Ni tukio la kihistoria katika maisha na hija ya Mama Kanisa. Imekuwa ni fursa makini kwa watu kutambua ubinadamu na maisha ya kiroho ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Wengi wameimarishwa katika imani kutokana na unyenyekevu unaofumbatwa katika maisha na imani.

Ikiwa kama Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alitoa ushuhuda thabiti wa imani yake mbele ya macho ya bahari ya watu duniani kutokana na imani na uvumilivu katika ugonjwa; Ratzinger kwa upande wake ametoa ushuhuda wa ushujaa unaofumbata utashi wa kukubali kwake kung'atuka kutoka madarakani kutokana na uzee, baada ya kufanya tafakari ya kina mbele ya Mwenyezi Mungu kuhusu dhamana na wajibu wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Viongozi hawa wawili wametoa mfano wa kuigwa si tu kwa njia ya Mafundisho yao, bali katika uhalisia wa maisha, uliopania daima kutafuta na kutekeleza mapenzi ya Mungu katika huduma na mazingira magumu ya maisha ya mwanadamu. Uamuzi wake wa kung'atuka kutoka madarakani si kitendo cha kukimbia utume na waamini waliokuwa wamekabidhiwa kwake kama Kiongozi mkuu. Ni mwaliko wa kuendelea kujiaminisha mbele ya Mungu na Kanisa, kwani Mungu mwenyewe ataendelea kuliongoza Kanisa lake.

Kwa unyenyekevu na utulivu wa ndani, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, anasema, amejitahidi kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya mafao ya Kanisa, ambalo ni mali ya Mungu linaloendelezwa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, ili kuishi, kukua na kuamsha dhamiri za watu. Kung'atuka madarakani kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ni mwaliko na changamoto ya sala na uwajibikaji wa wengi.

Kwanza kabisa ni dhamana na wajibu wa Makardinali waliopewa dhamana ya kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro, kama ilivyo pia kwa Kanisa zima linalopaswa kuwasindikiza Makardinali kwa njia ya sala ili kumchagua Papa Mpya atakayesimama kidete kutangaza Injili ya Kristo, kwa mafao ya Kanisa na Ulimwengu pamoja na kuiongoza Jumuiya ya Waamini kwa uaminifu wa Injili ya Kristo. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, Baba Mtakatifu peke yake hawezi kutekeleza yote!

Padre Federico Lombardi katika tahariri yake anasema, hata wao watafanya kwa kuungana na Baba Mtakatifu mstaafu anaendelea kusali na kutafakari kwa ajili ya Kanisa. Asante sana Baba Mtakatifu Benedikto XVI!







All the contents on this site are copyrighted ©.