2013-03-01 08:26:45

"Mimi si Khalifa wa Mtakatifu Petro tena! Bali Hujaji anayeanza hatua ya mwisho ya hija ya maisha yake hapa duniani"


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kabla ya kung'atuka rasmi kutoka madarakani hapo tarehe 28 Februari 2013, saa 2:00 Usiku, alipata fursa ya kusalimiana na waamini, mahujaji na wageni waliokuwa wamefurika kwa wingi kwenye Viunga vya Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo, nje kidogo ya mji wa Roma. Baba Mtakatifu alitokeza kwenye dirisha na kuwashukuru wote kwa upendo na mshikamano wanaomwonesha, ingawa wakati huu kuna hali tofauti kabisa na siku nyingine zilizotangulia.

Kwa unyenyekevu mkubwa, Baba Mtakatifu amesema, kuanzia saa 2: 00 Usiku, hatakuwa tena Khalifa wa Mtakatifu Petro, bali hujaji anayeanza hatua ya mwisho wa maisha yake hapa duniani. Anasema kwa: moyo,upendo, sala, tafakari na nguvu zilizoko ndani mwake, kuendelea kufanya kazi kwa ajili ya mafao ya Kanisa na Ulimwengu kwa ujumla. Anawaalika waamini na wote wenye mapenzi mema, kushikamana kwa dhati na Kristo kwa ajili ya mafao na ustawi wa Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, aliwapatia baraka zake za kitume na hatimaye kurejea ndani. Huu ukawa ni mwisho kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuonekana hadharani kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.