2013-02-28 12:09:53

"Nitakuwa mnyenyekevu na mtiifu kwa Papa Mpya"!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Alhamisi tarehe 28 Februari 2013 amekutana na kuzungumza na Makardinali kwa pamoja na baadaye, Makardinali walipata nafasi ya kuzungumza na Baba Mtakatifu mmoja mmoja kama alama ya kuagana naye! Baba Mtakatifu anawashukuru Makardinali kwa kufanya hija pamoja naye katika kipindi cha miaka minane, kwa pamoja wakitembea katika mwanga wa Kristo Mfufuka.

Anawashukuru kwa mawazo na ushauri waliompatia wakati alipokuwa anatekeleza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro na kwamba, katika kipindi cha miaka minane kwa pamoja wamefanya hija ya imani, kwa kutembea katika mwanga wa Kanisa, ingawa wakati fulani, kulikuwepo na wingu zito lililotanda kiasi cha kutishia maisha na utume wa Kanisa. Kwa pamoja wamejitahidi kulihudumia Kanisa la Kristo kwa imani, mapendo na sadaka kubwa; kwa kuwashirikisha waamini matumaini yanayobubujika kutoka kwa Kristo, wakakua na kukomaa katika umoja na mshikamano.

Baba Mtakatifu anawaomba Makardinali kushikamana katika utofauti wao, daima wakitamani kulitumikia Kanisa la Kristo, kwa kutambua kwamba, Kanisa ni Fumbo la Mwili wa Kristo, linalowashirikisha waamini wote katika ujumla wao, Kanisa ni hali halisi inayojionesha katika uhalisia wa maisha na moyo wa Kanisa ni Yesu mwenyewe na linaongozwa na nguvu ya Roho Mtakatifu. Liko duniani lakini si la dunia kwani Kanisa ni mali ya Fumbo la Utatu Mtakatifu.

Kanisa linaendelea kukua na kukomaa ili kuamsha roho za watu, kama ilivyokuwa kwa Bikira Maria kuweza kulipokea Neno la Mungu kadiri ya uwezo wa Roho Mtakatifu kwa kujitoa kikamilifu ili kupokea mpango wa Mungu, katika hali ya unyenyekevu na ufukara katika mchakato wa kumpeleka Kristo kwa watu! Baba Mtakatifu anawataka Makardinali kushikamana katika Fumbo la Maisha na Utume wa Kanisa; kwa sala, lakini zaidi katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, kama kielelezo cha huduma kwa Kanisa na Ulimwengu kwa ujumla.

Baba Mtakatifu amewahakikishia Makardinali kwamba, ataendelea kuwa karibu nao kwa njia ya Sala, hasa wakati huu wanapojiandaa kumchagua Papa Mpya, ili kuweza kusikiliza sauti ya Roho Mtakatifu kwa ajili ya Kanisa lake. Baba Mtakatifu anasema, atakuwa mwaminifu na mtiifu kwa Papa mpya!







All the contents on this site are copyrighted ©.