Juu ya Mwamba huu, Yesu anapenda kujenga na kulidumisha Kanisa lake
Ni katika dhana ya mwamba unaopatikana Kaisaria Filipi, uliotumika kwa ajili ya kutoa
heshima kwa miungu wa kipagani pamoja na Wafalme wa Kirumi, kama akina Erode Mkuu
na Kijana wake Filipo, kielelezo cha nguvu asilia, Yesu anautumia pia kwa ajili ya
Kujitambulisha kama Masiha atakayeteswa, kufa na kufufuka kutoka katika wafu, Mkombozi
wa dunia. Ni mwamba ambao unabubujika maji na kulowanisha uwanda wa Jangwa ili kuendeleza
zawadi ya uhai.
Hapa ndipo Yesu anawawauliza mitume wake, eti watu wanasema
kuwa Mwana wa Mtu ni nani? Na ninyi mnasema mimi ni nani?. Simoni anajibu kwa uhakika
kwamba, “Wewe ni Kristo Mwana wa Mungu aliye hai” Anatambua kwamba, amepata ufunuo
kutoka kwa Baba yake wa mbinguni. Juu ya mwamba huu, Yesu anajenga Kanisa lake, Maji
yanayobubujika kutoka mwambani hapo, yanakuwa ni kielelezo cha Sakramenti ya Ubatizo.
Kadiri ya Injili ya Yohane, Maji pia ni kielelezo cha kifo na ufufuko wa Bwana.
Ni mwanzo mpya wa kukutana, wa kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano utakaopata
utimilifu wake katika maisha ya uzima wa milele. Baba wa mbinguni anamtuma Mwanaye
wa Pekee aliyefichika machoni pa viumbe wengi, anaonekana sasa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu
katika maji yanayobubujika. Hapa umoja wa Fumbo la Utatu Mtakatifu unajionesha zaidi.