2013-02-27 07:57:37

Fanyeni maamuzi yenu kadiri ya Mwanga wa Injili


Yesu anaendelea hata leo hii kujenga na kuliimarisha Kanisa lake juu ya Mtakatifu Petro, Mwamba wa Kanisa, ambao kamwe hautaweza kushindwa na nguvu za kuzimu. Mwamba ulitumika sana katika ibada za Wapagani, lakini mwamba huu unapata maana mpya. Yesu alipofika pande za Kaisaria Filipi, aliwauliza wanafunzi wake, “watu wanasema kuwa ni nani?” Wakamjibu wengine wanasema kuwa ni Yohane Mbatizaji, wengine Elia, wengine Yeremia au mmojawapo wa Manabii.

Yesu akawauliza “Ninyi, Je, mnasema mimi ni nani?” Simoni Petro akajibu “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai” Yesu akasema, “Heri wewe Simoni mwana wa Yona, kwa maana hakuna binadamu yeyote aliyekufunuliajambo hili, ila Baba yangu aliye mbinguni. Nami ninakuambia wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga Kanisa langu; wala nguvu za kifo hazitaweza kulishinda. Nitakupa funguo za ufalme wa mbinguni; kila utakachofunga duniani, kitafungwa pia mbinguni; kile utakachofungua duniani, kitafunguliwa pia mbinguni. Mt. 16:13-19.

Padre Francesco Rossi de Gasper mtaalam wa Maandiko Matakatifu anasema, Kanisa la Kristo linachangamotishwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu inayojikita kwa Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, ili kuishi kwao kuwa ni ushuhuda wa Mungu anayeishi na kutenda kazi ndani mwao. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawaalika waamini na wote wenye mapenzi mema, kumfuasa Kristo wakiongozwa na Injili kama dir ana mwongozo wa maisha ya kila siku; daima wakiwa tayari kumwachia Mungu nafasi ya kuwaunda kadiri ya mpango wake, changamoto kwa waamini kufanya maamuzi yao mintarafu mwanga wa Injili.

Baba Mtakatifu anaendelea kusema, leo hii Wakristo hata kama amezaliwa, akaishi na kuelimishwa katika Jamii na Familia ya Kikristo, lakini hana budi kutoa nafasi ya kwanza kwa uwepo wa Mungu katika maisha yake, kama sehemu ya mchakato wa kupambana na vishawishi katika ulimwengu wa utandawazi.

Khalifa wa Mtakatifu Petro, anawaalika wale ambao wamepokea Mafundisho ya Kikristo, lakini bado hayajazamisha mizizi yake katika imani au pengine wamekengeuka, kuanza hija ya kumtafuta Yesu Kristo na Injili yake, kwa kujiandaa kutoka katika undani wa maisha kumkaribisha Mwenyezi mungu anayetaka kufanya makao katika moyo wa mwanadamu. Kutokana na ukweli huu, waamini hawana budi kuwa makini kiasi kwamba, hawachafuliwi na ndoto za mchana, mmwonekano wa nje au mali ya dunia hii.








All the contents on this site are copyrighted ©.