2013-02-26 10:06:47

Wasomi wanachangamotishwa kutumia uwezo wao wa kiakili kuimarisha imani katika matendo!


Padre Francois Xavier Dumortier Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian, kilichoko mjini Roma, anawaalika wanafunzi chuoni hapo kuungana na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa ajili ya kuliombea Kanisa ili liweze kupata mchungaji mkuu atakayeliendeleza baada ya Papa Benedikto wa kumi na sita, kung'atuka kutoka madarakani.

Kipindi kama hiki kinasheheni majonzi na simanzi, lakini kwa njia ya sala na tafakari ya kina, mwamini anaweza kutambua mpango wa Mungu katika hija ya maisha na utume wa Kanisa. Kanisa linapenda kumshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa utume wake kwa Kanisa katika kipindi cha miaka 8. Kama kielelezo cha shukrani kwa Baba Mtakatifu, wanafunzi wote wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregoriani watashiriki katika Katekesi ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, inayotarajiwa kufanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, siku ya Jumatano, tarehe 27 Februari 2013.

Katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro ameonesha umuhimu wa kumfuasa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu kwa njia ya huduma makini inayobubujika na kufumbata imani. Ni kiongozi ambaye ameonesha ujasiri na ukomavu wa kiimani; daima akajikita kutafuta ukweli kwa kutumia vyema vipaji na karama alizokirimiwa na Mwenyezi Mungu. Ameonesha dira kwa wafuasi wa Kristo kwamba, wanapaswa kumependa Mungu na jirani kama kielelezo cha imani tendaji. Ni kiongozi aliyekuwa na maneno machache, lakini yaliyogusa na kuacha chapa ya kudumu.

Kwa hakika Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amejitoa kimaso maso bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, akionesha fadhila ya unyenyekevu. Amekumbana na vikwazo na vizingiti vingi, lakini ameendelea kusimama imara kutokana na imani kwa Kristo na ujasiri katika ukweli. Alijitosa kulisafisha Kanisa la Kristo ili liendelee kuwa ni mchumba mwaminifu wa Kristo. Kanisa linaendelea kufanya hija ya maisha na utume wake kwa kuifuata ile Njia ya Msalaba, kwa kujikita katika fadhila ya unyenyekevu na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe kwa ajili ya watu wake.

Urithi ambao Baba Mtakatifu anapenda kuliachia Kanisa ni mapambano ya maisha ya kiroho, yanayomfungulia mwamini mlango wa imani thabiti. Kama Jumuiya ya Wasomi, wanaalika na Baba Mtakatifu kuhakikisha kuwa wanatumia kwa ukamilifu uwezo wao wa kufikiri na kutenda ili kuimarisha imani pamoja na kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Huu ni ujumbe wa imani unakumbatia Neno la Matumaini na maisha tele!







All the contents on this site are copyrighted ©.