2013-02-26 14:54:14

Wahamiaji na wageni watambuliwe, waheshimiwe na kuthaminiwa kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu


Kardinali Antonio Maria VegliĆ², Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi, Jumanne, tarehe 26 Februari, 2013 amekutana na kuzungumza na Kamati ya kiufundi ya Umoja wa Wafabiashara Wakristo nchini Italia.

Anasema, Mama Kanisa anopoadhimisha Jubilee ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, anapenda kukazia umuhimu wa waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kudumisha upendo na mshikamano wa dhati na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali mbali mbali za maisha.

Kanisa ni Sakramenti ya Umoja, kumbe, wahamiaji na wageni wajisikie kuwa ni sehemu ya Familia ya Mungu kwa kuwaonjesha umoja, upendo na mshikamano wa dhati unaobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe. Wote hawa wapokelewe kwa furaha, upendo na matumaini, ili kwa pamoja kujenga na kuimarisha Familia ya binadamu.

Katika ulimwengu wa utandawazi, Mama Kanisa bado anaendelea kuchangamotishwa kuhudumia kwa upendo, hasa wale wanaolazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na: maafa, njaa, vita, ukame na athari za mabadiliko ya tabianchi. Maendeleo ya sayansi na teknolojia yamewawezesha watu wengi kuwa karibu zaidi, changamoto ya kushirikiana kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi. Kuna mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kifedha yanayowafanya watu wengi kujisikia kuwa ni sehemu ya mchakato wa mabadiliko haya katika Jamii, kiasi cha kuvutwa kutoka sehemu moja hadi nyingine, kila mtu akiwa na sababu mbali mbali, wanakabiliana na vikwazo, lakini bado wanaendelea kusonga mbele kwa imani na matumaini.

Badala ya kufunga mipaka, kuna haja ya kuimarisha misingi ya haki za binadamu na kwamba, Kanisa katika Mafundisho yake Jamii linatambua kwamba, kila mtu anayo haki ya kuhama kutoka sehemu moja hadi nyingine katika harakati za kujitafutia maboresho ya maisha! Hii ni sehemu ya haki asilia. Wahamiaji wapewe ulinzi na kuhakikishiwa usalama wa maisha yao. Wahamiaji kwa upande wao, watambua urithi na tunu msingi za maisha ya kiroho na kijamii za wenyeji wao; wajitahidi kuheshimu sheria za nchi pamoja na kutekeleza dhamana na majukumu yao ya kila siku.

Pale inapowezekana Serikali za nchi husika ziboreshe hali na mazingira yatakayotoa hamasa kwa wananchi kubaki katika maeneo yao kwani haki ya kwanza kwa kila mtu ni kubaki katika nchi yake asilia. Athari za myumbo wa uchumi kimataifa, ukosefu wa mahitaji msingi, fursa za ajira, maafa asilia, kinzani na migogoro ya kivita, kijamii, kisiasa na kidini.

Haya ni kati ya matukio ambayo yameongeza wimbi la wahamiaji sehemu mbali mbali za dunia. Hapa Mama Kanisa anachangamotishwa kujikita katika Uinjilishaji Mpya, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu pamoja na matumizi sahihi ya maliasili kwa ajili ya mafao ya wengi. Wahamiaji waheshimiwe kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kamwe wasibaguliwe, kwani hata wao wanachangia pia katika ustawi na maendeleo ya nchi husika.

Mshikamano anasema Kardinali VegliĆ² una maanisha ile hali ya kuwajibika kwa kuwasaidia watu wanaoteseka katika shida na mahangaiko mbali mbali. Wahamiaji waheshimiwe na kuthaminiwa kwani ni nguvu kazi inayoweza kusaidia mchakato wa maendeleo katika nchi wahisani. Ni watu wenye heshima na utu wao, wathaminiwe. Kanisa kama chombo cha wokovu, liwashirikishe imani, matumaini na mapendo kwa kuwatambua kuwa ni sehemu ya Familia ya Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.