2013-02-26 09:36:28

Tafadhali sitisheni biashara ya silaha ili kuokoa maisha ya wananchi wa Syria


Patriaki Gregory wa tatu Laham wa Kanisa Katoliki Madhehebu ya Kigriki nchini Syria anaitaka Jumuiya ya Kimataifa kusitisha biashara ya silaha na Syria kwani madhara yake ni makubwa kutokana na vita ya wenyewe kwa wenyewe inayoendelea nchini humo. Watu wanaendelea kupoteza maisha yao na miundo mbinu kuharibiwa kwa sababu kuna kundi la wafanyabiashara linalofaidika kutokana na biashara ya silaha nchini Syria.

Patriaki Gregory wa tatu Laham anasema kwamba, umefika wakati kwa Jumuiya ya Kimataifa kuchukua hatua za dhati ili kuanzisha mchakato wa majadiliano ya kisiasa ili haki, amani na upatanisho viweze kutawala tena nchini Syria. Uchu wa faida kubwa kutokana na biashara ya silaha isiifanye Jumuiya ya Kimataifa kushindwa kuona mateso na mahangaiko ya wananchi wa Syria.

Anasema, Marekani na Russia ni wadau wakuu wa vita inayoendelea nchini Syria, wakiamua, wanaweza kusaidia kupata suluhu ya kudumu. Kanisa kwa njia ya sauti yake ya Kinabii pia linaalikwa kutekeleza wajibu wake ili amani ya kweli iweze kupatikana tena nchini Syria.







All the contents on this site are copyrighted ©.