2013-02-25 12:12:45

Watawa wa ndani wanaalikwa kusali kwa ajili ya kuliombea Kanisa katika kipindi hiki cha mpito!


Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, amewaandikia barua wakuu wa Mashirika ya Watawa wa ndani, kuwaomba kusali kwa ajili ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita pamoja na kuwaombea Makardinali watakaoshiriki kwenye mkutano wa kumchagua Papa mpya, ili waweze kuongozwa na Roho Mtakatifu, wakijitahidi kusoma alama za nyakati kwa Kanisa na Ulimwengu.

Baba Mtakatifu mwenyewe anaendelea kuwaomba waamini na watu wenye mapenzi mema, kumsindikiza katika sala anapoachia madaraka mikononi mwa Kristo mwenyewe, huku akiendelea kusubiri kwa imani na matumaini Papa mpya. Ni mwaliko wa pekee kwa Mashirika ya Watawa wa ndani kusali kwa ajili ya Kanisa, kwani sala za watawa zimelisindikiza Kanisa katika maisha na utume wake. Mkutano wa Makardinali unategemea sala na masifu ya watawa wa ndani.

Changamoto ya kujiachilia mikononi mwa Roho Mtakatifu kwa njia ya sala, ni mfano makini unaotolewa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ambaye kwa miaka nane ameliongoza Kanisa na kwa sasa anang'atuka kutoka madarakani, ili kupata muda mrefu zaidi wa kusali na kutafakari. Baba Mtakatifu kwa upande wake, anawashukuru watawa na kuwahakikishia kwamba, anathamini ushuhuda wao katika maisha na utume wa Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.