2013-02-25 07:36:17

Misingi ya Kanisa la Kristo


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati anatangaza kung’atuka kutoka madarakani aliwaambia waamini kwamba, analiaminisha Kanisa kwa mchungaji mkuu Yesu Kristo. Alisema kwamba, ana mang’amuzi na uhakika kwamba, Kanisa ni la Kristo atalipatia mchungaji mkuu kwa wakati wake.
Ni maneno yanayowakumbusha waamini utambulisho wa Kanisa kwamba, si kama taasisi nyingine nyingi zinazofahamika, bali hili ni Kanisa lililoanzishwa na Yesu Kristo mwenyewe, kama Jumuiya ya waamini ambayo imeendelea kufanya hija yake katika historia na sehemu mbali mbali za dunia, likitolea ushuhuda wa uwepo wa Mungu kati ya watu wake.
Hii ni sehemu ya kazi ya ukombozi iliyotekelezwa kuanzia kwa akina Ibrahim Baba wa Imani, Watu wa Agano la Kale na kupata utimilifu wake katika maisha ya Yesu wa Nazareti; Neno na Tukio muhimu linaonesha ufunuo wa Mungu, unaopania kuenzi utu, heshima na utimilifu wa maisha ya mwanadamu. Hii ni tafakari kutoka kwa Padre Francesco Rossi de Gasperis, mtaalam wa Maandiko Matakatifu anayependa kuwashirikisha waamini na watu wenye mapenzi mema ufahamu wa kina kuhusu Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa na umuhimu wa utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Kuna tofauti ya kubwa kati ya dini ya Kikristo na dini nyingine duniani. Kuna baadhi ya dini zinajitahidi kujenga uhusiano na Mwenyezi Mungu. Hizi ni jitihada za tafiti kuhusiana na Mungu na matokeo yake zinapata vielelezo, ibada. Lugha na sala kutokana na mahali pamoja na mazingira husika. Ukristo pia umepia hatua kama hii, lakini tofauti ni kwamba, hapa Mwenyezi Mungu ndiye anayeanza mchakato wa kumtafuta Mwanadamu, akimwonesha imani thabiti yenye mwendelezo kutoka kwa Ibrahim Baba wa Imani hadi kwa Yesu, akitoa mwaliko wa kuweza kujiunga naye ili aweze kumwinua.
Ukristo ni dini ya imani inayojikita katika Neno la Mwingiliano ambao umewezeshwa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu anayeimarisha hatua zote zinazochukuliwa na binadamu katika hija ya historia ya maisha yake, tangu pale katika kazi ya uumbaji hadi nyakati za mwisho. Yesu wa Nazareti ni Mwana wa Mungu aliyetwaa mwili, aliyeteswa, akafa na kufufuka. Hili ndilo Fumbo la Pasaka linalowaunganisha waamini katika hija ya kuyaendelea maisha ya uzima wa milele.
Yesu anaendelea kulijenga na kuimarisha Kanisa lake, hadi pale litakaposhiriki utukufu wa Kristo katika Yerusalemu ya mbinguni. Mwenyezi Mungu aliyefanya maagano na watu mbali mbali katika Maandiko Matakatifu ndiye anayeendelea kulitegemeza Kanisa lake kwa njia ya Khalifa wa Mtakatifu Petro, Mwamba hai ambalo unashikilia Kanisa la Kristo.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika kipindi hiki cha Kwaresima sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, anawaalika waamini kuchuchumilia toba na wongofu wa ndani, kwa kutoa nafasi kwa Mwenyezi Mungu ili kuweza kukabiliana na changamoto za maisha ya kila siku kwa imani na matumaini. Ni mwaliko wa kung’oa ndago za ubinafsi kwa kujishikamanisha na upendo kwa Mungu na jirani. Waamini wakumbatie Fumbo la Msalaba na kamwe wasing’ang’anie madaraka na mali za dunia bali kipaumbele kiwe ni kwa ajili ya kuendeleza kazi ya ukombozi iliyoanzishwa na Mwenyezi Mungu mwenyewe.
Kutubu na kuongoka anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, maana yake si kujitafuta mwenyewe wala nafasi katika Jamii, bali kuhakikisha kwamba, kila siku ya maisha ukweli, imani na mapendo kwa Mungu yanajidhihirisha. Wakati huu waamini wanaalikwa kufarijika na Neno la Mungu pamoja na neema zinazobubujika kutoka katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, zinazowapatia nguvu ya kumwita Mungu, Abba, yaani Baba.








All the contents on this site are copyrighted ©.