Upatanisho na haki ni misingi mikuu ya amani katika Jamii!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Waraka wake wa kichungaji, Dhamana
ya Afrika, Africae Munus anabainisha kwamba, upatanisho na haki ndiyo misingi mikuu
ya amani ambayo kimsingi ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, lakini inamshikirisha
mwanadamu katika maamuzi na vipaumbele vyake. Upatanisho na haki ni mambo yanyofumbatwa
katika ukweli na upendo. Hii ni changamoto kwa Familia ya binadamu kujipatanisha na
Mwenyezi Mungu pamoja na jirani. Wakristo wanaendelea kuchangamotishwa kuwa kweli
ni mfano wa kuigwa katika medani ya haki na upendo. Askofu Mkuu Josephat Lebulu,
wa Jimbo kuu la Arusha, katika Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea amani nchini
Tanzania iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Theresa wa Mtoto Yesu, hapo tarehe
20 Februari 2013 amesema, Wakristo wanao uwezo wa kulipiza kisasi dhidi ya mauaji
ya viongozi wao yanayofanywa na watu wasiopenda haki na amani, wanaotumiwa na watu
ndani na nje ya Tanzania, lakini Kristo, anawataka wasilipize kisasi ili kutompatia
shetani ushindi. “Sisi siyo wapumbavu na kwamba hatuwezi kufanya chochote…tunavutwa
tu na huruma ya Mwenyezi Mungu tukae kimya, lakini hakuna mwanadamu yeyote anayeweza
kuvumilia hili. Katika mazingira halisi ya kibinadamu, hakuna hata mmoja ambaye atafurahia
mauaji haya isipokuwa shetani na mawakala wake,” alisema. Askofu mkuu Lebulu anawaalika
Wakristo na waumini wa dini nyingine wenye mapenzi mema, wasitawaliwe na hasira, chuki
wala mioyo ya kulipa kisasi kwa sababu Yesu Kristo amewataka wasifanye hivyo, ingawa
uwezo wa kufanya hivyo wanao na haki ingekuwa upande wao. Alisema hayo katika mahubiri
yake ya Misa ya Wafu ya kumwombea marehemu Padri Mushi.
Askofu Mkuu Lebulu,
alisema: “Tusilipe kisasi, bali tushinde kwa yaliyo mema.” “Kama Mungu yupo nasi na
yupo upande wetu, hata kama kwa mabavu na bunduki, hakuna wa kututenganisha na upendo
wa Kristo. Je, ni dhiki, njaa, uchi, hatari au upanga,” alihoji na kuongeza: “Lakini
haya yote tunayashinda kwa Jina la Yesu na yeye anatupenda na hakuna chochote kitakachotutenga
na upendo wa Kristo.” Ibada hii ilihudhuriwa na umati mkubwa wa waamini na wapenda
amani Jimbo kuu la Arusha. Akizungumzia mauaji ya viongozi wa Kikristo nchini Tanzania
alisema, wanaamini ukweli wa mambo hayo utajulikana maana hakuna kinachotendeka kwa
siri ambacho hudumu hivyo hivyo bila kujulikana. Askofu Mkuu Lebulu, alisema Watanzania
wanalia kama watoto yatima kwa kukosa Baba au Wazazi na akaelezea kushangazwa kwake
kuhusu kauli za vitisho, matusi na kuleta hofu zilizokuwa zikisambazwa na baadhi ya
watu kwa njia za CD, DVD, kanda na ujumbe wa simu, huku vyombo vya usalama vikitazama
tu, halafu baadaye wanalalamika maadili yameshuka.
“Unashangaa vyombo vya usalama
vinaangalia tu, zipo kanda nyingi za matusi na vitisho dhidi ya waamini wa dini nyingine…vipo
wapi vyombo vya usalama kama wengine wanauawa namna hii. Mungu awaguse mioyo yao na
wabadilike na kumgeukia Mungu “Mambo hayo watu wa usalama wamezembea, tangu awali
kulikuwapo na viashiria vingi sana vya kuwapo hofu ya mauaji, lakini kwa nini hawashughulikiwi,
kisheria?” alihoji na kuongeza, “pengine hapa kuna siri imejificha.”
Alilaani
pia mauaji ya Mchungaji Mathayo Kachira (45), wa Kanisa la Pentekoste la Assemblies
of God, mkoani Geita, uchomaji moto wa makanisa na tukio la kumwagiwa tindikali kwa
Sheikh huko Zanzibar, kunakofanywa na baadhi ya watu kwa malengo wanayoyajua wao
wenyewe na akasema vitendo hivyo havisaidii kuleta amani, upendo na mshikamano wa
kitaifa. Kuna haja kwa watanzania kuanza mchakato wa kujenga misingi ya haki, amani
na upatanisho wa kitaifa, kwa kuzingatia kwanza kabisa mafao ya wengi pamoja na kujitahidi
kujenga mfumo wa haki jamii.