2013-02-22 11:23:43

Maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013


Vijana Wakatoliki kutoka Majimbo mbali mbali nchini China wameanza maandalizi ya kiroho yatakayowawezesha kushiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, itakayofanyika mjini Rio de Janeiro nchini Brazil, kuanzia tarehe 23 hadi tarehe 28 Julai 2013. Maandalizi yanayoendelea kwa sasa sehemu mbali mbali za dunia ni kuwawezesha vijana kujisikia kuwa kweli ni Wamissionari wanaotumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa Watu wa Mataifa, kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao adili na manyofu.
Vijana wanapaswa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kutambua kwamba, kama Wafuasi wa Kristo wanatumwa kutangaza Kweli za Kiinjili. Jumla ya vijana thelathini kutoka Jimbo kuu la Hong Kong Kao Po wanatarajiwa kuwa ni sehemu ya wajumbe watakaoshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani yanayokwenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Vijana watakaobaki Jimboni humo, wataungana na wenzao kiroho kwa shughuli mbali mbali zitakazopangwa na Idara ya Utume kwa Vijana.
Kanisa linataka kuwajengea vijana uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, wakitambua kwamba, wao ni jeuri na tumaini la Kanisa kwa sasa na kwa siku zijazo. Pale vijana hawa wanapojisikia kuwa na wito wa maisha ya Kipadre na Kitawa, wasisite kujitokeza mbele, tayari kuanza hija ya majiundo yatakayowawezesha siku moja kuwa ni wahudumu wa Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa na Matendo ya Huruma, yanayodhihirisha kwa namna ya pekee, Imani tendaji.








All the contents on this site are copyrighted ©.