2013-02-21 11:48:13

Umoja wa Mataifa wazindua "Mwaka wa Kimataifa wa zao la "Quinoa" katika mchakato wa kupambana na baa la njaa, utapiamlo na umaskini duniani


Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO, katika uzinduzi wa Mwaka wa Kimataifa wa Mazao ya Nafaka, kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, anasema, mazao ya nafaka yana mchango mkubwa katika mapambano dhidi ya baa la njaa, utapiamlo na umaskini duniani sanjari na kuhakikisha kwamba, kuna uhakika wa usalama wa chakula duniani.

Sherehe za uzinduzi huu zimehudhuriwa pia na Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa pamoja na viongozi wengine wa kisiasa. Anasema, zao la nafaka linalojulikana kama "Quinoa" lina utajiri mkubwa wa virutubisho vinavyohitajika katika mwili wa binadamu na kwamba, ni zao linaweza kustahimili ukame, hali mbali mbali za hewa na udongo na hivyo kusaidia katika mchakato wa mapambano ya baa la njaa na utapiamlo duniani.

Zao hili linaweza kuwa ni tegemeo kubwa la chakula bora kwa idadi ya watu inayozidi kuongezeka duniani, huku ikikabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na wasi wasi kuhusu hali ya usalama wa chakula duniani. Zao hili linaweza kuwa ni chakula mbadala kwa siku za usoni. Ni zao ambalo linaendelea kufanyiwa majaribio nchini Kenya na Mali na kwamba, majaribio ya awali yanaonesha kwamba, linaweza kustawi sehemu mbali mbali za dunia.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema, kati ya Malengo ya Maendeleo ya Millenia ni kuhakikisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inapunguza kwa kiasi kikubwa baa la njaa duniani; kwa kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula pamoja na kupambana na umaskini.







All the contents on this site are copyrighted ©.