China na Tanzania kuendeleza ushirikiano katika kuimarisha miundo mbinu!
Jamhuri ya Watu wa China imeendelea kuelezea dhamira yake ya kukuza ushirikiano na
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hususan katika sekta ya ujenzi. Balozi wa Jamhuri
ya Watu wa China nchini Tanzani Bwana Lu Younqing amefanya mazungumzo na Waziri wa
Ujenzi Dk. John Pombe Magufuli alipomtembelea ofisini kwake na kubainisha azma hiyo
ya kukuza ushirikiano kati ya nchi mbili hizi. Miradi mingi mikubwa ya ujenzi
hapa nchini imekuwa ikitekelezwa na makandarasi kutoka China. Makampuni hayo yamejikita
zaidi katika maeneo ya ujenzi wa barabara, majengo makubwa, miradi ya maji, kilimo
pamoja na miundombinu ya mawasiliano. Waziri wa Ujenzi akimshukuru Balozi huyo
kwa kumtembelea, amezipongeza kampuni za Kichina ambazo zinatekeleza miradi ya ujenzi
wa barabara, madaraja na majengo hapa nchhini kwa kuzitekeleza kazi hizo kwa ubora
unaoendana na viwango vilivyowekwa lakini kwa gharama nafuu. Hata hivyo, Waziri
Magufuli aliezea kuwepo kwa baadhi ya kampuni za Kichina ambazo utendaji wake hauridhishi
kwamba Wizara yake haitasita kuzichukulia hatua kali za kisheria na amemuomba Mheshimiwa
Balozi Younqing kushirikiana naye katika kuwafuatilia makandarasi wote watakaoanza
kulichafua jina zuri ambalo linaendelea kujengaka kwa makampuni ya ujenzi kutoka China.
Naye, Balozi Younqing akimhakikishia ushirikiano Waziri wa Ujenzi, pia amemuarifu
kwamba tayari maelekezo yametolewa kwa makandarasi wote wa Kichina wanaofanya shughuli
zao hapa Tanzania kuhakikisha kuwa pale inapowezekana wanatumia bidhaa na mali ghafi
zinazopatikana hapa nchini ikiwa ni pamoja na Wataalamu wa Kizalendo.