Viongozi wa Kanisa Kenya waendelea kuhimiza amani na utulivu
Wawakilishi kutoka chombo cha Kiekumeni cha makanisa Katoliki na Kianglikan Kenya,
wamerudia kutoa wito wa amani na mshikamano wakati wote wa uchaguzi mkuu na baada
ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi huo, unaofanyika tarehe 4 March mwaka huu.
Wawakilishi wametoa wito huo kwa nia za kuzuia umwangaji wa damu bure, kuzuia kilichotokea
baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2008.
Askofu Mkuu wa Kisumu, Zakayo Okoth
wa Jimbo Kuu la Kisimu akiwa mmoja wa wawakilishi hao amewasisitiza raia wa Kenya
kujiepusha na kuikataa roho ya ubinafsi na uchoyo , ambayo huleta uhasama, badala
yake wajenge moyo wa roho ya mshikamano na mazungumzo na maridhiano. Askofu Mkuu
Okoth alihitimisha kwa kutaja nia ya Kanisa Kenya kuingilia katika masuala ya kisiasa
kwamba hakuna jingine isipokuwa kujenga umoja na amani na mshikamano kwa Wakenya
wote."
Aidha katika waraka wa Kichungaji uliosainiwa na Rais wa Baraza la
Maaskofu Katoliki , Kardinali John Njue, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Nairobi, unasisitiza
kwamba, watu wa Kenya, ni mastahili yao kuishi kwa amani na utulivu, wakati wote
ukiwemo utendaji wote wa kisiasa na kijamii. Waraka huo unaonya, ili kuweza
kusitisha hali hii ya woga na wasiwasi wa machafuko, fujo na ghasia wakati wa chaguzi
za kisiasa , kila Mkenya anapaswa kuthamini maisha yake na maisha ya wengine na kuona
kwamba ni stahili ya kila Mkenya kushiriki katika uchaguzi kwa uhuru na haki, na uwezo
wa kupiga kura bila hofu wala vitisho. Amesema, "Tunataka wananchi wapate uelewe
wa waziwazi juu ya sheria mpya msingi zote zinazo tetea haki za Mkenya, badala
ya kutegemea maelezo toka kwa viongozi wa kisiasa."
Nae Askofu Mkuu Eliud
Wabukala, wa Kanisa la Kiaglikani Kenya, amekemea kila aina ya migawanyiko inayojengwa
katika misingi ya ukabila. Akitoa onyo hilo kwa mtazamo wa uchaguzi mkuu ujao, amehimiza
uongofu wa moyo kwa kila Mkenya, kuzama katika sala, kwa ajili ya uponyaji na upatanisho,
ili kuondokana na uchungu wa matukio ya siku za nyuma na mwendelezo vurugu. Amewataka
wasali kwa nia za kuomba umoja na amani, na kuvumiliana. “Huu ni wito wa maombi
ya dhati kwa taifa la letu, kwa viongozi, wenye mamlaka na wananchi. " Ameeelza hayo
kwa kurejea kwamba, mandhari ya amani barani Afrika, ni miongoni mwa mambo mengine
muhimu , yaliyojadiliwa katika Mkutano wa kwanza wa Ushauri ya Kianglikana na wa Baraza
la Wawakilishi wa majimbo Anglikana nchini Afrika, ambao ulifanyika katika Aprili
2011 mjini Nairobi, Kenya.
Askofu Mkuu Wabukala pia aliongeza kwamba, wakati
huu ni muafaka kupambanua na kuweka misingi ya maisha ya baadaye ya Wakenya. Na
hivyo ni mwaliko wa kuhakikisha kuwa Kenya, inaongozwa katika ngazi zote na wanaume
na wanawake wanyenyekevu, adilifu, walio wazi na wawajibikaji. Ni lazima, viongozi
hao wahakikishe kampeni zao za uchaguzi zinaepuka kila aina ya kauli za vitisho na
vitendo vinavyo weza kuhatarisha amani. Na hivyo Kanisa linatarajia mamlaka ya Serikali
inayosimamia zoezi la uchaguzi, ni muhimu kushikilia amani na kuhakikisha kwamba
wanasiasa wanafanya propaganda zao kwa kufuata sheria na katiba ya nchi. "