2013-02-20 11:28:41

Muasisi wa Mpango wa uzazi kwa njia ya asili afariki dunia!


Dr. Evelyn Livingston Billings, muasisi wa mpango wa uzazi kwa njia ya asili, amefariki dunia Jumamosi, tarehe 16 Februari 2013 akiwa na umri wa miaka 95. Dr Evelyn pamoja na mume wake Dr. John Billings kwa pamoja walianza mpango wa uzazi kwa njia ya asili, mpango ambao kwa wengi unajulikana kama "Billings".

Baada ya kufanya utafiti wa kina kuhusiana na zoezi la unyonyeshaji kwa wazazi pamoja na kuchunguza hali ya wanawake waliokuwa wanakaribia kipindi cha ukame, alifanikiwa kutoa mchango mkubwa katika maisha ya ndoa na familia. Kwa miaka hamsini, Madaktari hawa wametembelea sehemu mbali mbali za dunia ili kufundisha mpango wa uzazi kwa njia ya asili, mpango ambao unaungwa mkono na Mafundisho Jamii ya Kanisa kwa kuenzi Injili ya Uhai, dhidi ya Utamaduni wa kifo unaokumbatia sera za utoaji na vizuia mimba.

Kwa mara ya kwanza kitabu kuhusu mpango wa uzazi kwa njia ya asili kilitolewa kunako mwaka 1980, kikachapishwa kwa mara 16 katika lugha 22 za Kimataifa. Kwa mara ya mwisho kitabu hiki kimechapishwa kunako mwaka 2011. Dr. Evelyn aliwahi kuwa Mjumbe wa Taasisi ya Kipapa ya Maisha. Katika uhai wake alibahatika kupata watoto 9 na mmoja amekwisha fariki dunia. Ameacha wajukuu 39. Mume wake, Dr. John Billings alifariki dunia kunako mwaka 2007.







All the contents on this site are copyrighted ©.