2013-02-19 11:54:41

Ulinzi na usalama ni jukumu la raia wote!


Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya, Tanzania limetoa wito kwa taasisi binafsi na jamii kushirikiana na Jeshi hilo katika kuhakikisha wakazi wa Mbeya wanaishi kwa hali ya utulivu na amani kama wanavyoonesha ushirikianao tume ya haki na amani Jimbo Katoliki la Mbeya na hatimaye kutunukiwa hati ya ushirikiano mwema.

Akikabidhi vyeti kwa wadau mbalimbali wa ulinzi na usalama mkoani Mbeya Kamanda wa Polisi mkoani wa Mbeya, Diwani Athumani amesema jukumu la ulinzi na usalama ni la kila mtu, Serikali na sekta binafsi hivyo kila mmoja kwa nafasi yake anapaswa kuhakikisha mali na maisha ya kila mtanzania yanakuwa salama pamoja na mali zao.

Kamanda Diwani amesema Tume ya Haki na Amani, Jimbo Katoliki Mbeya ni miongoni mwa wadau muhimu wa ulinzi na usalama mkoani Mbeya katika kipindi cha mwaka 2012 na hivyo ametoa rai kuendelea kuwa wadau muhimu katika eneo hilo nyeti kwa mwaka 2013 hili kuendelea kulinda misingi hiyo iliyoachwa na hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kamabarage Nyerere.

Akipokea hati hiyo kwa niaba ya Askofu Evaristus Chengula wa Jimbo Katoliki la Mbeya, Katibu wa Tume ya Haki na Amani Jimbo la Mbeya, Sabinus Malima amelishukuru Jeshi la Polisi kwa kutambua na kuona umuhimu wa tume hiyo ambayo imekuwa ikitoa elimu kwa waumini wake wa kanisa katoliki kuhusu umuhimu wa haki, amani, upendo na mapatano.

Amesema Kanisa Katoliki kupitia Tume yake ya Haki na Amani ina jukumu kubwa ambalo imekuwa ikilifanya tangu awali la kutoa elimu kwa waumini wake na jamii kwa ujumla kuhusu faida ya nchi kuwa tulivu na kwamba Tume inaamini kuwa bila amani na utulivu watanzania kupitia imani zao hawataweza kupata wasaa wa kupumzika,kutulia na kuabudu na kumwamini mwenyezi mungu.

Malima amesema nchi ama watu wanaoingia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe hawataweza kupata wasaa wa kuingia Makanisani ama Misikitini kwani, vita inapita hata katika nyumba za ibada na hivyo kila kukicha na kila dakika iendayo kwa mungu watu wanakuwa wakikaa na kuhangahikia migogoro, malumbano, vurugu, kujiokoa na makando kando mengine ambayo hayampendezi Mwenyezi Mungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.