Rais Shein akutana na Askofu Augustino Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar kufuatia mauaji
ya kinyama ya Padre Evarist Mushi
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein, amepokea
kwa mshtuko mauaji ya Padri Evarist Mushi na kutoa pole kwa waumini, ndugu jamaa,
marafiki na wananchi wote wa Zanzibar kufuatia kifo hicho.
Waziri wa Nchi Ofisi
ya Makamo wa Pili wa Rais Mohamed Aboud ameeleza hayo Jumatatu, Februari 18, 2013
na kusisitiza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Jeshi
la Polisi itawasaka hadi kuwatia mikononi na hatimaye kuwafikisha kwenye vyombo vya
sheria wale wote waliohusika na mauaji hayo.
Waziri Aboud ameyaeleza hayo
wakati alipozungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Vuga, kwa niaba ya Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein kufuatia mauaji
ya Padri Evarist Mushi wa Jimbo Katoliki Zanzibar Parokia ya Mtakatifu Joseph, Shangani.
Jumapili,
Dk. Shein alikutana na Askofu Augustino Shao wa Kanisa Katoliki, Jimbo la Zanzibar,
huko katika Ikulu Ndogo Migombani, Zanzibar na kueleza masikitiko yake kutokana na
mauaji hayo ya Padri Mushi wa Kanisa Katoliki la Zanzibar, na kuelezea haja ya kuwepo
kwa uvumilivu katika kipindi hichi cha msiba.
Katika mazungumzo na waandishi
wa habari, Waziri Aboud alisema kuwa Serikali imejipanga vizuri kupitia vyombo vyake
vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha kuwa watu wote waliohusika na mauaji hayo wanakamatwa
mara moja. “Kutokana na jiografia ya Zanzibar, Tunaelewa kwamba zipo sehemu katika
kisiwa cha Zanzibar ambazo wahalifu wanaweza kuzitumia, hivyo Jeshi la Polisi kwa
kushirikiana na vyombo husika vitaziba mianya yote ili kupambana na uhalifu “, alisema
Aboud.
Matendo ya uhalifu yanafanywa katika mazingira ya usiri mkubwa kwa hivyo
ili wahalifu hao wakamatwe wananchi hawana budi kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi
pale wanapohitajika. Akijibu suali la Mwandishi, Mhe.Aboud alikanusha taarifa zilizozagaa
mitaani za kuwepo silaha nyingi mikononi mwa watu wasiohusika na kuwataka wananchi
kuondoa hofu.
Sambamba na hayo, Mhe. Aboud amewataka viongozi wa dini
mbali mbali pamoja na waumini wa dini zote hapa Zanzibar kuwa wastamilivu katika
kipindi hiki kigumu cha maombolezi. Aidha, Waziri Aboud alisisitiza haja ya kuwepo
uvumilivu kwa waamini wa dini zote ili kuirejesha Zanzibar katika historia yake ya
kutokuwa na migongano ya kidini.