2013-02-19 10:12:21

Maaskofu Katoliki wako Zanzibar kushiriki katika Ibada ya Kumwombea Marehemu Padre Evarist Mushi!


Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Tanzania, Jumatano, tarehe 20 Februari 2013 watakusanyika kusali kwa ajili ya kumwombea Marehemu Padre Evarist Mushi aliyeuwawa kikatili Jumapili, tarehe 17 Februari, 2013 wakati akienda kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu. Hii pia itakuwa ni nafasi ya kusali kwa ajili ya kuombea amani na utulivu nchini Tanzania kutokana na vitendo vya madhulumu ya kidini vinavyofanywa dhidi ya Wakristo.

Taarifa kutoka Dar es Salaam zinabainisha kwamba, kuna idadi kubwa ya Maaskofu Katoliki Tanzania wanaotarajia kuhudhuria mazishi ya Padre Evarist Mushi (55), kama kielelezo cha mshikamano wa imani, katika kipindi hiki cha madhulumu ya kidini. Waamini na watu wenye mapenzi mema wanasubiri kusikia tamko la Baraza la Maaskofu kuhusu madhulumu ya kidini na uchinjaji wa nyama jambo ambalo pia limepelekea hivi karibuni mauaji ya Mchungaji Mathew Kachira, katika Kitongoji cha Buselesele, Katoro, Mkoani Geita.

Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam akizungumzia juu ya mauaji ya Padre Evarist Mushi wa Jimbo Katoliki Zanzibar anasema, hili ni tukio la kupangwa, kwani kama vyombo vya ulinzi na usalama vingeweza kuwa makini kidogo, mauaji haya yasingalitokea. Vipeperushi na mihadhara ya kashfa za kidini inayoendeshwa na Kikundi cha Uamsho ni kielelezo tosha kabisa. Vyombo vya ulinzi na usalama vinafahamu kwa hakika kile kinachoendelea nchini Tanzania.

Kardinali Pengo anasema, mauaji ya Padre Evarist Mushi yametokea wakati anakwenda kutekeleza shughuli zake za kichungaji. Kifo chake si tu pigo kwa Kanisa Katoliki bali ni kwa Taifa zima la Tanzania na wapenda amani wote. Vitendo vya chokochoko na madhulumu ya kidini visipodhibitiwa kikamilifu, Tanzania inaweza kujikuta pabaya. Jambo la msingi kwa watanzania ni kujenga na kudumisha moyo wa uvumilivu, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Kardinali Pengo anasema, kuna haja ya kuombea amani na utulivu pamoja na kuelezana ukweli, utakaowaweka huru. Askofu msaidizi Eusebius Nzigilwa wa Jimbo kuu la Dar es Salaam anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea amani, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yosefu, Jimbo kuu Dar es Salaam, majira ya jioni.







All the contents on this site are copyrighted ©.