2013-02-18 11:43:25

Tamko la Jukwaa la Kikristo mkoani Mbeya kuhusu mauaji ya viongozi wa Kikristo Tanzania


Viongozi wakuu wa Wakristo mkoani Mbeya wametoa tamko zito kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia mfulululizo wa matukio ya mauaji ya viongozi wa dini na vurugu zinazoendana na vita ya kiimani kuwa ni matokeo ya serikali kuendelea kukumbatia sera za udini Jukwaa la Wakristo mkoani Mbeya linaundwa na Waamini wa Kanisa Katoliki, Baraza la Makanisa ya Kikristo Tanzania pamoja na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania na kutolewa tarehe 18 Februari, 2013 mbele ya waandishi wa habari katika ukumbi wa Kanisa la Pentekoste, Jijini Mbeya. Jukwaa la Wakristo linasema, Serikali imelifumbia macho suala la udini na sasa madhara yake yanaanza kujionesha kwa kasi ya ajabu!

"Ushahidi wa CD na DVD za Sheikh Ilunga ndiyo matokeo haya lakini Serikali ni kama imebariki vitendo hivi na leo tumeshuhudia Padre Evaristi Mushi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Minazi Miwili Zanzibar ameuawa kwa kupigwa risasi, Mchungaji Mathayo Kichila wa Geita aliyechinjwa, Padre wa Kanisa Katoliki Zanzibar aliyepigwa risasi mwezi Desemba, Makanisa yamebomolewa na vitu vya thamani kuharibiwa, lakini Serikali ipo kimya,"alisema Katibu wa Jukwaa hilo. Askofu Damianos Kongoro wa Kanisa la Pentekoste.

Alisema kwa nini wasite kusema kwamba serikali inaibeba dini ya Kiislamu kwa kuwa jukumu la Serikali ni kuhakikisha wananchi wote wanaishi kwa amani na utulivu lakini haipo hivyo kwa Serikali ya awamu ya nne. Limesema sehemu ya tamko hilo kuwa mshukiwa wa kwanza anayejuwa kila kitu ni Sheikh Ilunga aliyesambaza CD na DVD kuhusu mikakati ya kuwauwa Wachungaji, Mapadre na Maaskofu na matokeo yake yameanza kuonekana lakini bado yupo huru na madhara yameanza kujitokeza.

"Serikali inatushangaza kwa viongozi wa kikristo wakiuawa na kufanyiwa vurugu inasema ni wahuni lakini wakifanyiwa unyama viongozi wa kikristo inasema tuvumiliane wakati mchungaji ameuawa Buserere mkoani Geita na kikundi kinachodhaniwa ni wanaharakati wa Kiislamu wenye jazba na ghadhabu kali inayodaiwa kutokana na mvutano wa wakristo na waislamu kuhusu nani mwenye haki kisheria kuchinja nyama, hatua zilizochukuliwa haziridhishi wala kukidhi matakwa ya wananchi wapenda amani,"walisema.

Wametolea mifano ya Mwenyekiti wa CCM Rungwe, John Mwankenja aliyeuawa baada ya kupigwa risasi kwa mambo yanayodhaniwa ni ya kisiasa Serikali ilichukuwa hatua madhubuti na kutuma wachunguzi kutoka Dar es Saalam na wananchi waliridhika na uchunguzi huo iweje kuchukulia kiurahisi suala la viongozi wa kikristo.

"Ili wakristo wote nchini warudishe imani yao kwa Serikali mambo yafuatayo ni lazima yachukuliwe hatua za haraka iwezekanavyo: Serikali izingatie utawala wa sheria kulingana na ahadi yake katika kushughulikia masuala ya kijamii na siyo vinginevyo. Suala la kuuwa lisichukuliwe kama mazoea na inapotokea Serikali lazima ichukuwe hatua stahiki kwa kuzingatia utawala wa sheria, tunataka serikali itueleze ni ushahidi gani zaidi inayoutaka kuliko ule uliopatikana kwenye CD na DVD zilizotolewa na sheikh Ilunga kama kweli inazingatia utawala wa sheria," wamesema.

Wameongeza "tunataka serikali iwajibike kutolea ufafanuzi kauli ya waziri wa Nchi Steven Wasira inayohusu haki ya kuchinja kwa Waislamu kama inatokana na sheria gani ya nchi, kama serikali inatekeleza utawala wa sheria tunataka Wakristo tuwe na machinjio na bucha zetu kulingana na imani yetu,"

Viongozi hao wamesema kama Serikali haitachukuwa hatua za makusudi katika kutekeleza madai yao kama viongozi wa dini ya kikristo watachukuwa hatua ya kuwaambia waumini wao kwamba Serikali inakumbatia dini ya kiislamu na wao watajuwa la kufanya.

Hata hivyo Maaskofu hao wamesema pamoja na kutaka utekelezaji wa haraka kutoka kwa serikali bado wamewaomba Wakristo wawe katika hali ya maombi na utulivu kwa wakati huu ambapo wapo katika vita ya kiroho ili Mwenyezi Mungu awaimarishie amani na utulivu, zawadi kubwa kutoka kwake na ambayo ni nguzo ya taifa na kwamba tamko hili rasmi la Jukwaa la Wakristo mbeya lisomwe katika makanisa yote siku ya Jumapili Febrauri, 24, 2013.

Tamko hilo limesomwa kwa Mkuu wa Mkoa kwa naiaba ya Rais ambapo nakala zimesambazwa kwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya,Tanzania Christian forum Taifa,Mwenyekiti wa the Tanganyika Law Society, Wabunge wa Mkoa wa Mbeya na Vyombo vyote vya Habari mkoani Mbeya.








All the contents on this site are copyrighted ©.