Rais Jakaya Mrisho Kikwete amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya kuuawa
kwa Padri Evarist Mushi wa Parokia ya Minara Miwili, Jimbo Katoliki Zanzibar mauaji
yaliyotokea Zanzibar, Jumapili tarehe 17 Februari 2013. Rais Kikwete anawapa pole
nyingi na rambirambi za dhati kwa Askofu Augustino Shayo wa Jimbo Katoliki, Zanzibar,
maaskofu wote nchini na waamini wote wa Parokia ya Minara Miwili kwa msiba huo mkubwa
uliowakuta. Rais kikwete amemwambia Askofu Shayo. ”Napenda kuwahakikishia kuwa
tupo pamoja katika kuomboleza kifo cha Mpendwa Marehemu Padri Evarist Mushi na kuwa
msiba huu ni wa kwetu sote.” Ameongeza Rais Kikwete: “Nimeliagiza Jeshi la Polisi
nchini kukusanya nguvu zake zote na maarifa yake yote kuhakikisha kuwa uchunguzi wa
kina na wa haraka sana unafanyika ili kubaini mhusika ama wahusika na kuwakamata ili
kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria.” “Aidha, nimewaagiza Jeshi la Polisi washirikiane
na vyombo vingine vya Usalama nchini na mashirika ya upepelezi ya nchi rafiki katika
kufanya uchunguzi wa mauaji haya.” Amesisitiza Rais Kikwete: “Nataka ukweli wake
ujulikane ili kama kuna jambo lolote zaidi liweze kushughulikiwa na kukata mzizi wa
fitina.” Vile vile, Rais Kikwete amewataka waamini wa Kanisa Katoliki na wananchi
wote kuwa watulivu wakati Serikali inashughulikia suala hili na kuwa hakuna mtu wala
watu ama kikundi cha watu kitachoruhusiwa kuvuruga amani ya Tanzania.