2013-02-16 09:14:43

Baba Mtakatifu Benedikto XVI: Mjumbe wa amani!


Maaskofu Katoliki kutoka Mashariki ya Kati wanamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa kuwa bega kwa bega na Kanisa Mashariki ya Kati, nyakati za shida na magumu, daima akiwahimiza kujisikia kuwa ni sehemu ya Kanisa na kwa ajili ya Kanisa na kwamba, walikuwa wanalo jukumu la kusonga mbele kwa imani na matumaini bila ya kukatishwa tamaa na magumu wanayokabiliana nayo katika kuwahudumia Watu wa Mungu, huko Mashariki ya Kati.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa mara nyingine tena ameonesha ukweli, busara na unyenyekevu wa hali ya juu kwa kutamka kwa utashi na uhuru kamili kwamba, anang'atuka kutoka madarakani. Maaskofu kutoka Mashariki ya Kati wanamshukuru na kumpongeza wanasema, wataendelea kumsindikiza katika awamu ya pili ya maisha yake kwa njia ya sala.

Ni kiongozi ambaye amesimama kidete kulinda na kutetea: haki na amani; utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Ameng'atuka kutoka madarakani si kwa kushinikizwa kama ambavyo baadhi ya watu wanataka kuwasadikisha watu wengine, bali kutokana na upendo na mafao ya Kanisa.

Ni mfano ya mfanyakazi mnyenyekevu katika Shamba la Bwana anayetambua uwezo wake, kiasi hata cha kudiriki kuachia dhamana yake kama kiongozi mkuu, ili kutoa nafasi kwa kiongozi mwingine mwenye nguvu, ari na kasi kubwa zaidi kuendeleza utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Maaskofu Katoliki Mashariki wanamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuitisha, kuadhimisha na hatimaye, kuwapatia Waraka wa Kichungaji, Kanisa Mashariki ya Kati, "Ecclesia in Medio Oriente". Ni Sinodi iliyopania kujenga na kuimarisha misingi ya haki, amani, upendo na utulivu kwa kutambua kwamba, wote ni watoto wa Mungu na tofauti zao ziwe ni kichocheo cha kushikamana na wala si kwa ajili ya kuwagawa! Wananchi wanaoishi Mashariki ya Kati wanapaswa kujikita katika mchakato wa haki, amani na upatanisho. Waamini waendelee kutolea ushuhuda wa imani katika matendo.

Maamuzi yaliyofanywa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, yataendelea kuwa rejea kwa watu waliopewa dhamana ya uongozi ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla, kuchunguza dhamiri zao kwa unyenyekevu mbele ya Mwenyezi Mungu na kuangalia jinsi wanavyotekeleza majukumu yao ikiwa ni kadiri ya mapenzi ya Mungu au ni kwa kujitafuta wao wenyewe na masilahi na utukufu binafsi.

Viongozi wajifunze kutafuta mafao ya wengi wanapotekeleza wajibu na dhamana yao ndani ya Jamii. Viongozi watambue kwamba, wamepewa wajibu wa kuhudumia na wala si kuhudumiwa!







All the contents on this site are copyrighted ©.