2013-02-15 07:54:19

Watanzania Roma watoa heshima zao kwa Ibada ya Misa ya wafu kwa Marehemu Alphonsina Shayo.


Alhamisi hii majira ya saa tano za asubuhi , Watanzania Roma walishiriki katika Ibada ya Misa ya Wafu kwa nia ya kutoa heshima zao za mwisho na kuiombea Roho ya Marehemu Alphosina Anselmi Shayo, aliyefariki hapa Roma wiki iliyopita.

Ibada hiyo, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Dorothea, ikiongozwa na Padre Felix Mushobozi wa Shirika la Damu Takatifu ya Yesu , akishirikiana na Mapadre wengine ya kadhaa, pia ilihudhuriwa na makumi ya Masista wa mashirika mbalimbali na walei kadhaa akiwepo mwakilishi wa Ubalozi Bwana Mbilinyi.

Marehemu Alphosina alifaki dunia , Mapema Alhamis 6 Februari 2013, baada ya kupita muda wa saa kadhaa, tangu alipowasili Roma Jumatano, akitokea Arusha Tanzania, kwa lengo la kushiriki katika sherehe ya kuweka nadhiri za daima, mdogo wake, Sista Maria Blanca Shayo. Sherehe iliyofanyika Siku ya Jumamosi 9 Feburari 2013. Sherehe iliyomhusu pia Sista Maria Basilisa Puka, wote wawili wakiwa ni Masista wa Shirika la Sakramenti Takatifu, wazawa wa Moshi Tanzania. Kifo cha Alphonsina Shayo, kimebaki kuwa kitendawili.

Padre Felix Mushobozi katika homilia yake, ametahadharisha, hakuna anayejua wakati wala mahali, au kwa namna gani kifo kitamfika au kuepushwa nacho isipokuwa Mungu peke yake. Ametahadharisha kifo hakijali hadhi, cheo, umri wala jenda. Hivyo basi, kila kinapotokea, unakuwa ni mwaliko mpya kwa walio hai, kuwa tayari, wakati wowote, tunapoitwa kuhitimisha hija ya maisha duniani.

Nae kiongozi wa Jumuiya ya wanafunzi Katoliki Roma, alitoa shukurani zake za dhati kwa ushirikiano mzuri ulioonyeshwa na Watanzania tangu Msiba huu ulipotokea. Wengi wameshiriki kwa namna moja au nyingine kupitia sala, faraja na rambirambi na kusaidia katika kufanikisha taratibu za mwili wa Marehemu kurudishwa nyumbani. Amesema mshikamano na umoja huu uzidi kuwa ngao na utambulisho wa Watazania mahali popote walipo.

Mara baada ya Ibada hii, Mwili wa Marehemu Alphonsina ulipelekwa Uwanja wa Ndege wa Roma , tayari kwa kusafirishwa mapema Ijumaa hadi Tanzania.Marehemu ameacha Mme na watoto wawili.
Tunamwombea pumziko la Milele, Amina.








All the contents on this site are copyrighted ©.