2013-02-15 08:07:18

Vijana nchini Brazil wanachangamotishwa na Baba Mtakatifu kujitosa kweli kweli kuwatangazia wenzi wao Injili inayokoa!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita amewaandikia Maaskofu Katoliki Brazili wakati huu wa Kampeni ya Kwaresima kwa Mwaka 2013 inayoingia katika maadhimisho ya miaka hamsini tangu ilipoanzishwa.

Anasema, Kipindi cha Kwaresima ni muda muafaka wa kusali, kutubu na kufanya matendo ya huruma kama njia mahususi ya kujiandaa kikamilifu katika maadhimisho ya Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, kwa kujielekeza zaidi katika maandalizi ya Siku ya Vijana Duniani, itakaofanyika mjini Rio de Janeiro kuanzia tarehe 23 hadi tarehe 28 Julai 2013. Kauli mbiu inayoongoza maadhimisho haya ni udugu na vijana, kama changamoto kwa vijana nchini Brazil kujitosa kimaso maso kuitikia wito kutoka kwa Mwenyezi Mungu, wakisema bila kusita, “mimi hapa Bwana, nitume” kama alivyosema Nabii Isaya.

Baba Mtakatifu anasema, anapenda kujiunga na Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil, kwa kuwapatia baraka na neema kwa wadau wote wanaojitoa bila ya kujibakiza ili kufanikisha Kampeni hii ya Kipindi cha Kwaresima, kama sehemu ya mchakato wa kuwawezesha vijana kuwa wajenzi wa Jamii inayosimikwa katika haki na udugu mintarafu kweli za Kiinjili. Alama za nyakati zinajionesha ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla kwa njia ya vijana, ikiwa kama fursa hizi zinazojitokeza hazitaweza kutumiwa kikamilifu, Kanisa na Jamii inaweza kupoteza fursa ya kuleta wongofu wa ndani. Vijana ni tumaini la leo na kesho iliyo bora zaidi.

Baba Mtakatifu anasema, Kanisa linapenda kuwaona vijana wakishiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa kwa njia ya Jumuiya zao, hali wakionesha matumaini waliyo nayo ndani mwao kwa Kanisa. Dhamana hiii nyeti inawahitaji viongozi na walezi wanaotoa kipaumbele cha kwanza kwa katika majiundo ya vijana, wakiwaonesha dira na njia ya kufuata bila ya kuwawekea vikwazo; wajenge mshikamano wa dhati, kwa kushuhudia kwamba: wokovu na imani pamoja na ufuasi wa Yesu Kristo ni mambo yanayorutubishwa kila siku ya maisha.

Vijana nchini Brazil wanahamasishwa na Baba Mtakatifu kutafuta maana ya maisha yao kwa njia ya tafakari ya Injili ya Yesu Kristo, kwa kujenga urafiki, ili hatimaye, kujipatia kile kilicho bora na kinachoweza kuwaokoa kutoka katika utumwa wa dhambi na mauti kama Mwenyezi Mungu alivyomsafisha Nabii Isaya kwa kaa la moto, akawa safi, tayari kujitosa kimaso maso kutangaza Neno la Mungu.

Vijana wanapokutana na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yao, wanapata fursa ya kuonja mabadiliko ya ndani, kiasi hata cha kuweza kujitokeza kwa ajili ya kuwatangazia vijana wenzao Habari Njema ya Wokovu; kugundua Jangwa na utupu wa maisha ya kiroho unaowaandama vijana wa kizazi kipya, ili hatimaye, waweze kupokea yale mambo ya msingi tu!

Injili na Imani ya Kanisa ni mambo muhimu sana yaliyojadiliwa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, kama inavyobainisha pia Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Vijana waonje ile furaha ya kumwamini Kristo; wamfuate katika hija ya maisha yao, hali wakimtolea ushuhuda katika hali mbali mbali wanamoishi, ili kuweza kutangaza utajiri wa imani kwa Kristo na Kanisa lake. Baba Mtakatifu, anawatakia kheri na baraka wananchi wa Brazil, lakini zaidi vijana wa kizazi kipya, akiwaweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Aparecida.








All the contents on this site are copyrighted ©.