2013-02-15 09:28:14

Matunda ya Jubilee ya Miaka 100 ya Chuo cha St. Albert, India


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu wakati wa ziara yake ya kichungaji nchini India, ameshiriki pia katika Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 100 tangu Chuo cha Albert kilichoko Ranchi, kilipoanzishwa. Katika kipindi chote hiki, kimebarikiwa kupata Mapadre: 2000; Maaskofu na Maaskofu wakuu 35 pamoja na Kardinali mmoja.

Hiki ni kati ya vyuo maarufu sana vinavyotoa majiundo makini, Kaskazini mwa India. Kimekuwa mstari wa mbele katika kuwaandaa wadau wa uinjilishaji nchini India, watu ambao wamekuwa msaada mkubwa katika mikakati na shughuli za Uinjilishaji na utamadunisho, ili kuhakikisha kwamba, viongozi wa Kanisa wanafahamu fika tunu msingi za kitamaduni na Kiinjili, ili kuweza kutekeleza barabara majukumu yao ya kichungaji.

Hii ndiyo dira ya Kanisa katika mikakati ya majiundo kwa Majandokasisi pamoja na kuhakikisha kwamba, Seminari na nyumba za malezi zinapata walezi makini, wenye sifa na vigezo vinavyohitajika kwa ajili ya majiundo ya viongozi wa Kanisa kwa sasa kwa siku za usoni.

Waseminari wanapaswa kujifunza pamoja na kukuza ari na moyo wa kimissionari, tayari kujitoa kimasomaso kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia. Watambue kwamba, wanapaswa katika maneno na matendo yao kuwa ni Kristo mwingine kwa wale wanaowahudumia. Viongozi wa Kanisa wajitahidi kusoma alama za nyakati, kwani dunia inabadilika kwa kasi ya ajabu!

Kardinali Filoni katika hotuba yake kwa Waseminari chuoni hapo anakazia kwamba, Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, uwasaidie kumfahamu, kumpenda na kumhudumia Kristo, aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu; utume ambao wanapaswa kuutekeleza kwa ari na moyo mkuu, daima wakijitahidi kuwa ni watu wa imani.

Waonje na kuguswa na mifano iliyotolewa na Mababa wa Imani wanaosimuliwa katika Maandiko Matakatifu. Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu pamoja na Mitume ni vielelezo makini sana vya imani katika maisha na utume wa Kanisa.

Kipindi cha malezi kiwasaidie kunoa akili na mioyo yao barabara, tayari kuwatumikia Watu wa Mungu bila kujibakiza. Ili kufanikisha azma hii, kuna haja kwanza kabisa kuwani watu wa Sala wanaofanya tafakari ya kina kuhusu Neno la Mungu pamoja na kushiriki Sakramenti za Kanisa, kwa namna ya pekee, Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Upatanisho. Kipindi cha majiundo kitumike vyema ili kujipatia ujuzi na maarifa yatakayowasaidia kutekeleza shughuli zao za kichungaji kwa siku za usoni.

Kardinali Filoni anawaalika Majandokasisi: kutambua na kuthamini kwa namna ya pekee fadhila ya utii, useja na ufukara wa Kiinjili kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Ufalme wa Mungu. Maisha ya Sala na Sadaka yawawezeshe kuvuka vikwazo, majaribu na vishawishi kwa kukimbilia daima huruma ya Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho.

Familia ya Mungu inahitaji viongozi waaminifu, waadilifu, wachapa kazi na wachamungu, wanaoonesha ushuhuda wa: imani, matumaini na mapendo katika uhalisia wa maisha. Uhuru wa ndani, uwajengee moyo wa upendo na mshikamano kwa ajili ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.