2013-02-15 14:43:38

FAO inamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa kusimama kidete kupambana na baa la njaa na umaskini duniani


Bwana Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO katika mahojiano na Radio Vatican anasema kwamba, amepokea kwa mshangao mkubwa taarifa za kung'atuka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kutoka madarakani kutokana na uzee.

Anamshukuru na kumpongeza kwa uamuzi unaoonesha hekima na busara inayoleta changamoto kubwa kwa kutambua udhaifu wa mwili na hatimaye, kung'atuka ili kiongozi mwingine aweze kuendeleza Jahazi la Mtakatifu Petro, yaani kuliongoza Kanisa.

FAO inasema kwamba, Kanisa limekuwa mdau mkubwa katika mapambano dhidi ya baa la njaa na umaskini duniani. Kwa kufuata mfano na Mafundisho Jamii ya Kanisa, FAO imeweza kujiwekea sera na mikakati ya kutokomeza baa la njaa nchini Brazil na Serikali ikafanikiwa. Kwa sasa Jumuiya ya Kimataifa inaelekeza nguvu zake Barani Afrika. Ni matumaini ya FAO kwamba, Papa atakayechaguliwa ataendeleza sera na mikakati ya kupambana na baa la njaa pamoja na umaskini duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.