2013-02-14 09:07:50

Marehemu Askofu Amedeus Msarikie alisoma alama za nyakati katika kuleta maboresho katika sekta ya elimu Tanzania, leo Mwenge kinafunika!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika waraka wake "Dhamana ya Afrika" anabainisha kwamba, shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki ni raslimali yenye thamani kubwa katika kujifunza na kujenga mshikamano, umoja na utulivu katika Jamii, kwani wanafunzi wanafundishwa tunu hizi tangu wakiwa wadogo, wakirithishwa pia tunu bora za maisha ya Kiafrika sanjari na tunu za Kiinjili. RealAudioMP3

Ni mahali ambapo Jamii inajifunza na kujenga utamaduni wa majadiliano ya kidini na kiekumene, sanjari na kunoa akili na mioyo ya vijana wa kizazi kipya katika mwanga wa Injili pamoja na kuwa tayari kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha ya watu Barani Afrika, ili Bara la Afrika liwe ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Maneno haya yanasikika kwa mara nyingine tena, wakati huu Kanisa Katoliki Tanzania linapompumzisha katika usingizi wa amani, Marehemu Askofu mstaafu Amedeus Msarikie wa Jimbo Katoliki Moshi, aliyefariki dunia hivi karibuni wakati akipata matibabu Jijini Nairobi. Kabla ya mwili wake kurudishwa Jimboni Moshi, siku ya tarehe 13 Februari 2013 kwa ajili ya maziko, Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumwombea Marehemu Askofu mstaafu Msarikie.

Mwili wake ulipofikishwa mjini Moshi, ulipelekwa kwenye nyumba ya Mapadre wazee Longuo, mahali ambapo, Marehemu Askofu Msarikie aliishi tangu alipong'atuka kutoka madarakani. Ilikuwa ni fursa ya kuweza kuagana na Mapadre wazee na wagonjwa ambao kutokana na hali yao hawataweza kuhudhuria Ibada ya Misa na Mazishi ya Askofu mstaafu Msarikie yanayofanyika kwenye Kanisa kuu la Kristo Mfalme.

Askofu mkuu Yuda Thadeus Ruwaichi wa Jimbo kuu la Mwanza, aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na kuwakumbusha waamini waliohudhuria katika Ibada hii kwamba, Fumbo la Kifo linamshirikisha mwamini uhai wa Kristo mwenyewe. Marehemu Askofu Msarikie atakumbukwa kutokana na matumizi bora ya vipaji alivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu, yaani: imani, matumaini, ukarimu na majitoleo kwa watanzania wengi. Anawaalika waamini na wote wenye mapenzi mema kuendelea kumsindikiza kwa njia ya imani.

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro anasema kwamba, kwa taaluma Marehemu Askofu Msarikie alikuwa ni mwalimu aliyebobea, mwenye uwezo, uzoefu na mang'amuzi mapana. Alitumia vipaji hivi kukabiliana na changamoto ya kushuka kwa kiwango na ubora wa elimu Tanzania.

Akapania kuanzisha Chuo cha Ualimu, kitakachowaandaa walimu watakaowafundisha vyema watoto wa watanzania kwa juhudi, maarifa na weledi. Huo ukawa ni mwanzo wa Chuo cha Ualimu cha Mtakatifu Yosefu, ambacho kimepanuka na sasa ni Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mwenge, kinachopania kuwa kweli ni mwanga wa dunia "Lux Mundi". Askofu Mkude anasema, mwanzoni baadhi ya Maaskofu walionesha wasi wasi kutokana na ugumu na changamoto za kuwa na Chuo cha Ualimu.

Askofu Msarikie hakukata tamaa, bali alisonga mbele, akakabiliana na changamoto hizi kwa imani na matumaini, leo matunda yake yanaonekana, amefariki dunia, lakini watakaochota elimu na maarifa kutoka Chuo Kikuu cha Mwenge, bila shaka watakuwa ni mwanga wa mataifa katika Jamii.

Hii ndiyo changamoto ambayo Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania limejifunza na leo hii Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augostino cha Tanzania SAUT kimekuwa ni kinara kwa vyuo vikuu nchini Tanzania. Marehemu Askofu Msarikie alisoma alama za nyakati katika maboresho ya elimu Tanzania, kwa hakika ataendelea kukumbukwa kutokana na mchango wake kwa maisha ya kiroho na kiutu miongoni mwa watanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.