2013-02-14 07:45:51

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Uingereza: Katekesi ya kina na ushuhuda makini wa tunu msingi za Kiinjili


Baraza la Maaskofu katoliki Uingereza, hivi karibuni liliwakusanya wadau wa Uinjilishaji kutoka Majimbo mbali mbali nchini humo, ili kuweza kufahamiana, kusali na kulitafakari Neno la Mungu pamoja; kupeana ari na moyo wa kuweza kusonga mbele kwa imani na matumaini katika dhamana ya Uinjilishaji mpya, ajenda inayovaliwa njuga na Mama Kanisa, katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani. RealAudioMP3

Kongamano la kwanza liliwahusisha waamini walei kutoka katika vyama mbali mbali vya kitume na kongamano la pili liliwajumuisha Makleri kutoka Uingereza. Ilikuwa ni fursa makini ya kuweza kusikiliza shuhuda kutoka kwa viongozi wa Kanisa na waamini walei walioshiriki katika maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Uinjilishaji Mpya, iliyofanyika hivi karibuni mjini Vatican. Makongamano yote haya mawili yalikuwa na uwakilishi mkubwa, uliopewa dhamana ya kufikisha yale yaliyojadiliwa, kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Wajumbe katika makongamano yote mawili wanasema kwamba, changamoto kubwa iliyoko mbele yao kwa sasa kabla ya kujimwaga uwanjani kumtangaza Kristo, wanapaswa kwanza kabisa kujiinjilisha wao wenyewe kwa kujichotea utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, Mafundisho Jamii ya Kanisa, Biblia na Nyaraka za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ambazo kwa hakika zina utajiri mkubwa katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu; kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mungu na binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Katekisimu ni nyenzo muhimu sana katika kuifahamu na kuiungama Imani inayopaswa kujionesha katika matendo adili. Katika mahubiri yake, Askofu Seamus Cunnigham wa Jimbo Katoliki la Hexham na Newcastle, Uingereza alizungumzia kuhusu umuhimu wa Sakramenti ya Ubatizo kama mlango unaomwezesha mwamini kushiriki: ukuhani, ufalme na unabii wa Kristo. Kutokana na dhamana hii, kila mwamini anao wajibu wa kurithisha imani na kutangaza Habari Njema ya Wokovu; kwa maneno machache, kila mwamini anaalikwa na Mama Kanisa kujitosa kimaso maso katika azma ya Uinjilishaji wa mtu mzima.

Askofu Cunnigham anaonya kwamba, kabla mwamini hajaweza kujimwaga barabara kwenye Jukwaa la Uinjilishaji, anapaswa kwanza kabisa yeye mwenyewe kujiinjilisha, kwa kujenga uhusiano wa karibu zaidi na Yesu Kristo, aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu kama yanavyonena Maandiko Matakatifu. Waamini wajibidishe kumfahamu, kumpenda na kumtumikia, ili waweze kuonja upendo na huruma yake isiyokuwa na kifani. Kwa kujichotea nguvu kutoka kwa Kristo, waamini nao wataweza kuwashirikisha jirani zao, ule ushuhuda unaobubujika kutoka katika Imani tendaji.

Mwamini anaweza kujenga uhusiano wa dhati na Yesu Kristo kwa njia ya sala, tafakari ya Neno la Mungu, Maisha ya Kisakramenti yanayomwezesha kupata neema na baraka anazohitaji katika hija ya maisha yake ya kiroho. Nguvu na neema hii inapatikana kwa namna ya pekee kabisa katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, mahali ambapo, mwamini anajifunza kujitoa na kujimega kwa ajili ya jirani zake, kama Kristo mwenyewe alivyofanya pale Mlimani Kalvari.

Hakuna haja ya kuogopa kujitosa katika Uinjilishaji, kwani Kristo amewaahidia wafuasi wake kwamba, atakuwa nao bega kwa bega na kwa njia ya uwepo wa Roho Mtakatifu. Kuna haja ya kujenga utamaduni wa kudumu katika sala, tafakari na ukimya ili kumsikiliza Kristo anayeongea kutoka katika undani wa maisha ya mwamini.

Askofu Cunnigham anasema inasikitisha kuona kwamba, kuna misululu mirefu ya waamini wanaokwenda kupokea Ekaristi Takatifu, lakini ni waamini wachache sana wanaopokea Sakramenti ya Upatanisho, inayomwonjesha mwamini upendo na huruma ya Mungu isiyokuwa na kifani. Kutoshiriki katika sakramenti hii ni dalili za mwamini kufilisika katika maisha ya kiroho na matokeo yake, atapotelea kwenye ombwe kwani mwamini kama huyo atakuwa na dhamiri mfu isiyoweza kupembua mema ya kufuata na mabaya ya kuachana nayo, kama njia ya kujishikamanisha na Kristo.

Wajumbe wa Makongamano haya wanasema, ulikuwa ni wakati uliokubalika kwa kusali kwa dhati, kutafakari kwa kina, kuabudu Ekaristi takatifu katika hali ya Ibada na uchaji mkuu. Waamini walipata pia fursa ya kushirikishana mang’amuzi ya imani, vikwazo na vipaumbele vinavyotolewa na Mama Kanisa wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ili kila mwamini aweze walau kufaidika na maadhimisho haya.

Tukio hili limewakumbusha wengi, changamoto iliyotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipowataka waamini kujifunga kibwebwe katika azma ya Uinjilishaji Mpya katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.








All the contents on this site are copyrighted ©.