2013-02-14 08:09:26

Familia ya Mungu yaungana na Benedikto XVI kuanza kipindi cha toba na wongofu wa ndani!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatano ya Majivu, jioni, tarehe 13 Februari 2013, ameadhimisha Ibada ya Misa takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kama mwanzo wa kipindi cha Kwaresima. Waamini walikusanyika kuzunguka Kaburi la Mtakatifu Petro ili kuomba maombezi yake kwa ajili ya hija ambayo Kanisa linafanya kwa sasa, kwa kuuisha imani kwa Kristo mchungaji mkuu.

Kwake, imekuwa ni fursa ya pekee kwa ajili ya kuwashukuru waamini wa Jimbo kuu la Roma anapokaribia kuhitimisha utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, anawaomba kuendelea kumkumbuka katika sala zao.

Mama Kanisa katika kipindi hiki cha Kwaresima anawaalika waamini kwa namna ya pekee, kutubu na kuongoka; kwa kufunga na kusali, kwa kujiachia huru kabisa ili kutoa nafasi ya uwepo wa Mungu katika hija ya maisha yao, daima wakijitahidi kuikimbilia huruma yake, kwani Mungu ni mwingi wa huruma na wala si mwepesi wa hasira. Kumrudia Mungu ni jambo linalowezekana kwani hiki ni kitendo cha neema, ikiwa kama mwamini mwenyewe anakubali kushirikiana na neema ya Mungu.

Ni mwaliko wa kusimama kidete kupambana kufa na kupona na makwazo pamoja navitendo vyote vinavyomnyima mwanadamu haki zake msingi. Mabadiliko haya yanapaswa kufanyika katika undani wa moyo wa mwamini mwenyewe, jambo ambalo si rahisi linahitaji ujasiri mkuu, kwa kuchunguza dhamiri na nia, ili kumwachia Mungu nafasi ya kuweza kuleta mabadiliko pamoja na kumkirimia mwamini wongofu wa ndani, jambo ambalo linahusisha Jumuiya nzima ya waamini; alama makini ya imani na kama kielelezo cha maisha ya Kikristo.

Kristo amekuja duniani ili kuwaunganisha watu kwa njia ya imani, mwaliko kwa kila mwamini kutekeleza dhamana hii, hasa wakati huu wa kipindi cha Kwaresima. Mchakato wa toba ya kweli, unafanywa na Jumuiya ya Waamini ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu katika mahubiri yake, anaendelea kukazia umuhimu wa ushuhuda wa imani katika maisha ya waamini, kama njia ya kuonesha ile sura ya Kristo, ambayo wakati mwingine inachafuliwa na waamini wenyewe; kwa kukosa umoja na mshikamano; utengano na misigano katika Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Kwaresima ni mwaliko wa kudumisha umoja wa Kikanisa, kwa kuondokana na ubinafsi, chuki na uhasama, kama kielelezo cha unyenyekevu kwa wale ambao wako mbali na imani au wamekengeuka.

Kwaresima ndio wakati uliokubalika, unapaswa kutumiwa kikamilifu, kama alivyofanya Kristo mwenyewe kwa kujinyenyekesha, kiasi cha kuteswa, kufa na kufufuka kutoka katika wafu, ili kuweza kumpatanisha mwanadamu na Muumba wake kwa njia ya Fumbo la Msalaba. Katika mateso na mahangaiko ya mwanadamu, Mwenyezi Mungu anasema Baba Mtakatifu anaonesha ile hali ya kuhesabiwa haki.

Kwaresima kiwe ni kipindi cha kumrudia Mungu kwa moyo wote, kwa kufuata ile Njia ya Msalaba kwa kujitoa bila ya kujibakiza. Ni mwaliko wa kila mwamini kujitambua kwamba ni zawadi safi mbele ya Mwenyezi Mungu, mwaliko wa kujitoa katika ubinafsi ili kumpatia Mungu nafasi ya kuishi na kutenda. Kwaresima kiwe ni kipindi cha kusikiliza kwa makini Neno la Mungu linaloangaza mapito ya miguu ya waamini.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anabainisha kwamba, Mama Kanisa anawahamasisha watoto wake wakati wa Mfungo wa Kwaresima: kujinyima, kusali na kufunga kama sehemu ya mchakato wa mwamini kumrudia Muumba wake. Yote haya yafanyike katika hali ya unyenyekevu bila ya majivuno wala mtu kupenda kujikweza, kama ambavyo Yesu mwenyewe anavyokemea.

Ushuhuda wa matendo ya huruma utapata thawabu yake mbele ya Mwenyezi Mungu; mwaliko kwa sasa ni kuendelea kuambatana naye katika imani, ili baada ya maisha ya hapa duniani; katika mwanga wa amani waweze kuonana naye uso kwa uso.

Katika kipindi cha Kwaresima anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, changamoto kubwa iliyoko mbele ya waamini ni kutubu na kumwongokea Mungu; kwa kupokea neema yake, waamini wanaweza kuwa wapya na hatimaye, kushiriki katika maisha angavu ya Kristo. Majivu yawakumbushe waamini changamoto ya kutubu na kuongoka!








All the contents on this site are copyrighted ©.