2013-02-13 14:22:36

Kanisa ni la Kristo na kamwe hataliacha pweke, bali atalipatia Kiongozi pamoja na kuendelea kulihudumia!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kabla ya katekesi yake, Jumatano tarehe 13 Februari 2013 kwa waamini na mahujaji waliokuwa wamemiminika kwa wingi mjini Vatican kwa ajili ya kusikiliza Katekesi yake, aligusia juu ya uamuzi alioufanya wa kung'atuka kutoka madarakani, dhamana aliyokuwa amekabidhiwa kunako tarehe 19 Aprili 2005. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu anasema kwamba, amefanya uamuzi huu kwa utashi na uhuru kamili kwa ajili ya mafao ya Kanisa, baada ya kusali kwa muda mrefu pamoja na kuchunguza dhamiri yake mbele ya Mwenyezi Mungu, huku akitambua uzito wa maamuzi yake. Anatambua kwamba, kutokana na uzee hawezi tena kutekeleza wajibu wake kikamilifu kama Khalifa wa Mtakatifu Petro; nguvu ambazo kimsingi zinahitajika. Anasema anauhakika kwamba, Kanisa ni la Kristo na kamwe hataweza kuliacha pweke bila ya kulipatia Kiongozi pamoja na kulihudumia.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amechukua fursa hii kuwashukuru waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwa upendo na sala ambazo wamemsindikiza nazo katika kipindi chote cha uongozi wake. Anawaomba kuendelea kusali kwa ajili ya Papa mpya na Kanisa ana uhakika kwamba, Bwana ataliongoza Kanisa lake.







All the contents on this site are copyrighted ©.