2013-02-13 07:11:24

Kanisa limempoteza kiongozi makini katika maisha, kazi na wito wake!


AskofuTarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya mazishi ya Askofu mstaafu Amedeus Msarikie wa Jimbo Katoliki Moshi, aliyefariki dunia hivi karibuni. RealAudioMP3

Mahubiri kadiri ya taarifa kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania yatatolewa na Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo Kuu la Arusha na Askofu Isaac Amani wa jimbo Katoliki Moshi, ataongoza Ibada ya Maziko ya Askofu Amedeus Msarikie. Habari zaidi zinabainisha kwamba, Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, ameongoza Ibada ya Misa takatifu kwa ajili ya kumwombea Marehemu Askofu Msarikie kabla ya kusafirishwa hadi Jimboni Moshi.

Rais mstaafu Benjamini William Mkapa ni kati ya viongozi wakuu wa Serikali wanaohudhuria mazishi ya Askofu Msarikie kwa kutoa heshima zao na baadaye kushiriki katika Ibada ya Masifu ya Jioni. Kwa upande wa Kanisa, Kardinali Polycarp Pengo na Balozi wa Vatican nchini Tanzania wanatarajiwa kuhudhuria kadiri ya taarifa kutoka Jimbo Katoliki Moshi.

Akizungumza na Radio Vatican, Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro anasema, Kanisa la Tanzania limempoteza kiongozi makini katika maisha, kazi na wito wake; mtu aliyependa kusimamia dhana ya ukweli na uwazi; pamoja na utekelezaji wake. Alikuwa ni mtu mwenye kutoa na kupokea ushauri kutoka kwa wengine.

Askofu Mkude anasema kwamba, alianza kumfahamu wakati ambapo Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili alipotembelea Tanzania, hapa alionesha uwezo mkubwa katika kupanga, kusimamia, kuratibu na kutekeleza yale yaliyokuwa yameamriwa. Waamini na watu wenye mapenzi mema wanapoomboleza kifo cha Askofu Msarikie wanapaswa kutambua kwamba, ni kiongozi aliyejenga maisha na utume wake kwa katika Mwamba thabiti ambao ni Yesu Kristo, aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani yaliyotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, iwe ni fursa kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuenzi yale mambo msingi ambayo Marehemu Askofu Msarikie aliyasimamia na kuyatekeleza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Watanzania kiroho na kimwili. Kama Askofu aliwafundisha, akawaongoza na kuwatakatifuza watu wake, mwaliko na changamoto ya kurithisha zawadi ya Imani kwa watoto na vijana wa kizazi kipya, ili Bwana atakapokuja aweze kuikuta imani ikiwa bado ipo!








All the contents on this site are copyrighted ©.